• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 1:29 PM
Mabadiliko ya sheria ya SRC yaibua hofu

Mabadiliko ya sheria ya SRC yaibua hofu

Na IBRAHIM ORUKO

HOFU imekumba Tume ya Mishahara (SRC) baada ya Rais Uhuru Kenyatta kutia sahihi mabadiliko ya pamoja ya sheria inayompa mamlaka ya kuteua mwenyekiti wa tume hiyo.

Rais Kenyatta aliidhinisha mabadiliko hayo Ijumaa na yanaathiri sheria ya SRC, Sheria ya Pensheni na sheria ya kudhibiti dawa na sumu.

Kufuatia mabadiliko katika sheria ya SRC, makamishna wa tume hiyo hawatakuwa wakihudumu kwa muda na rais atakuwa na mamlaka ya kumteua mwenyekiti.

Hata hivyo, kuna wasiwasi katika SRC kuhusu uhalali wa hatua hiyo na gharama ya utekelezaji wa mabadiliko hayo.

Wafanyakazi wa tume wanahofia kuwa uamuzi wa kuwafanya makamishna wafanyakazi wa kudumu unaweza kupingwa mahakamani kwa msingi kuwa idadi yao inazidi iliyowekwa kikatiba.

Wasiwasi wa wafanyakazi hao ni kuwa tume itahitaji ofisi kubwa kutosheleza makamishna wa kudumu na wafanyakazi zaidi kuajiriwa katika ofisi zao.

SRC ina makamishna 11 wanaowakilisha taasisi tofauti.

Wanawakilisha Tume ya Huduma ya Bunge, Tume ya Mahakama, Seneti, Baraza la Usalama, Muungano wa Vyama wa Wafanyakazi (Cotu), Shirikisho la Waajiri Kenya (FKE) na shirika la wataalamu.

Wengine ni Waziri wa Fedha, Mwanasheria Mkuu na waziri wa utumishi wa umma.

Makamishna hao huwa wanahudumu kwa kipindi kimoja cha miaka sita na hawawezi kuteuliwa tena. Kwa sasa, shughuli ya kuteua makamishna wapya inaendelea baada ya kipindi cha iliyoongozwa na Sarah Serem kumalizika mwaka 2017.

Ingawa sheria ya SRC inataja taasisi zinazofaa kutoa makamishna, katiba inasema kila tume huru inapaswa kuwa na makamishna wasiozidi tisa.

“Tuna wasiwasi na uwezo wa tume kwa sababu kufuatia sheria iliyotiwa sahihi na rais sasa itatubidi tuhame ofisi zetu za sasa,” alisema afisa mmoja wa cheo cha juu wa tume hiyo ambaye aliomba tusimtaje jina kwa sababu haruhusiwi kuzungumza kwa niaba ya tume.

Alisema itabidi tume ipate ofisi kubwa na kuajiri wafanyakazi zaidi kwa sababu kila kamishna atahitaji kuwa na karani, msaidizi wa kibinafsi na dereva.

Kiranja wa walio wachache katika bunge Junet Mohammed anaunga makamishna wa muda kwa sababu jukumu lao ni la kutoa ushauri.

“Kazi yao kuu ni kushauri serikali kuhusu mishahara na masharti ya kazi ya watumishi wa umma. Baada ya kufanya hivyo, watakuwa wakifanya kazi gani? aliuliza.

 

You can share this post!

Pwani yaapa kujisuka upya kuingia serikalini 2022

Mvua yazuia mashahidi wa kesi ya Konza City kufika kortini

adminleo