• Nairobi
  • Last Updated April 16th, 2024 6:11 PM
Ford Kenya na ANC wakosa kuafikiana

Ford Kenya na ANC wakosa kuafikiana

Na SHABAN MAKOKHA

MGAWANYIKO umezuka kati ya viongozi wa chama cha Ford Kenya na ANC kuhusu mtindo wa kuwachagua viongozi wao wakuu iwapo vyama hivyo vitaunganishwa viwe chama kimoja.

Vyama hivyo tayari vimeanzisha mchakato wa kuunganishwa kwa lengo la kuwaleta pamoja jamii ya waluhya wakilenga uchaguzi mkuu wa mwaka wa 2022.

Naibu Kiongozi wa chama cha Ford Kenya Boni Khalwale aliashiria kwamba Kiongozi wa ANC Musalia Mudavadi ndiye atateuliwa kiongozi wa chama kitakachobuniwa kwa kuwa ni mkubwa kiitifaki kuliko Bw Moses Wetangula.

Hata hivyo Katibu Mkuu wa Ford Kenya Dkt Eseli Simiyu alikataa wazo hilo.

“Hatujashauriana vilivyo kuhusu swala hili la kuunganisha vyama vyetu. Fikira zisizofaa zinazohujumu mpango huo hazifai kwa wakati huu,” akasema Dkt Simiyu.

Katibu huyo wa Ford Kenya aliungwa mkono ma mwenzake wa ANC Godfrey Osotsi ambaye pia alikataa pendekezo la Bw Mudavadi kupewa uongozi wa chama.

Wawili hao walisema usimamizi unaoshughulikia maswala ya muungano wao haujajadili swala la nani atakiongoza chama na kuongeza kwamba ni mapema sana kuangazia swala hilo.

“Bado tuko katika hatua ya mwanzo katika kuunganisha vyama vyetu. Lakini hatujajadili kuhusu wale watakaoshikilia nyadhifa mbalimbali chamani,” akasema Dkt Simiyu.

Kwa upande wake Bw Osotsi alipuuzilia mbali hatua ya kuunganisha vyama hivyo akisema ni ajenda inayosukumwa na watu wachache wenye nia ya kufaidika kibinafsi na kisiasa.

Aliongeza kwamba muungano unaopendekezwa unakosa ajenda ya kudumu na wanachama wengi wa vyama husika hawajashauriwa wala kuhusishwa akisisitiza umoja wa jamii ya Waluhya unatumiwa tu kama kisingizio na viongozi wakuu.

Akihutubu katika mazishi kijijini Eshikhoni kaunti ndogo ya Navakholo, Dkt Khalwale alisisitiza kwamba jamii ya Mulembe imejipanga vizuri kuliko miaka ya nyuma ili kutoa mwaniaji mmoja wa kutwaa kiti cha urais mwaka wa 2022.

Dkt Khalwale alimlaumu Katibu Mkuu wa muungano wa vyama vya wafanyikazi(COTU) Francis Atwoli kutokana na kauli aliyotoa wakati wa sikukuu ya Leba kwamba katiba inafaa kurekebishwa ili kumpa Rais Uhuru Kenyatta nafasi mpya ya uongozi baada ya kustaafu mwaka wa 2022.

“Hakuna haraka ya kufanya mabadiliko ya kikatiba ili kuwanufaisha watu wachache kwa kuwapa nyadhifa za uongozi. Rais Kenyatta anafaa kukataa pendekezo hili,” akaseama Dkt Khalwale.

Kulingana naye mabadiliko kwa katiba yatamwezesha Rais Kenyatta kupata wadhifa wa waziri mkuu mwenye mamlaka amubwa na naibu wake akiwa Seneta wa Baringo Gideon Moi huku Raila Odinga akiutwaa wadhifa wa urais.

 

 

 

 

You can share this post!

Wanaosaka ajira ughaibuni watahadharishwa dhidi ya ugaidi

Kalameni amtoroka slay queen akihofia hasara zaidi

adminleo