• Nairobi
  • Last Updated April 24th, 2024 10:08 PM
Mbunge alala ndani kwa kushambulia mfanyabiashara

Mbunge alala ndani kwa kushambulia mfanyabiashara

Na WYCLIFFE MUIA

MBUNGE wa Bunge la Afrika Mashariki, Simon Mbugua, alilala seli Jumanne pamoja na watu wengine watatu wanaoshukiwa kuhusika katika uvamizi wa aliyekuwa mwenyekiti wa wafanyabiashara jijini Nairobi, Timothy Muriuki.

Jumanne, maafisa wa ujasusi walimuwinda Bw Mbugua na kumkamata katika hoteli ya Sagret jijini Nairobi na baada ya kumhoji saa kadhaa wakamuweka ndani na anatarajiwa kufikishwa mahakamani.

Mbunge huyo alikamatwa pamoja na washukiwa wengine Anthony Otieno Aboo almaarufu Jamal, Solomon Benjamin Onyango almaarufu Solo na mshukiwa mwingine aliyekuwa nao katika hoteli ya Sagret.

Mkuu wa Ujasusi katika Kaunti ya Nairobi Ireri Kamwende aliongoza kikosi cha maafisa kadhaa kumkamata mbunge huyo.

“Tutamhoji zaidi ili aweze kutusaidia kujua ukweli kuhusu uvamizi huo wa mfanyabiashara,” alisema Bw Kamwende.

“Tulifanikiwa kuwakamata Jamal na Solo lakini wenzao watatu bado wako mafichoni. Tuna uhakika tutawakamata pia,” alisema Kamwende.

Washukiwa hao wengine ni Brian Owino almaarufu Orange, Michael Mbanya na Suleiman Hussein almaarufu Rescue.

Wananume hao watano walinaswa wakimvamia vikali Bw Muriuki kabla ya kumtimua katika hoteli moja jijini Nairobi alipokuwa akitoa taarifa kwa wanahabari kuhusu hali ya uongozi wa jiji la Nairobi.

You can share this post!

Sura mpya ya ‘Baba’ baada ya salamu

Polisi waonya huenda Al-Shaabab watekeleze uvamizi Ramadhan

adminleo