• Nairobi
  • Last Updated April 19th, 2024 6:55 PM
Ajuta kumbaka mpenziwe wa zamani

Ajuta kumbaka mpenziwe wa zamani

Na BENSON MATHEKA

MWANAMUME aliyekabiliwa na shtaka la kumbaka mpenzi wake wa zamani, alipatikana na hatia ya kumshambulia mwanadada huyo na kutozwa faini ya Sh30,000.

Paul Angweny atafungwa jela mwaka mmoja iwapo hatalipa faini hiyo aliyotozwa na Hakimu Mkuu Mwandamizi wa Kibera Barbara Ojoo. Mahakama haikumpata na hatia ya kumbaka mwanamke huyo ilivyodaiwa lakini ikampata na hatia ya kumjeruhi kimaksudi.

Angweny aliambia mahakama kwamba, mwanamke huyo alikuwa mpenzi wake wa zamani lakini akakanusha kwamba alifanya mapenzi naye bila hiari yake akimtisha kwa kisu.

Ilidaiwa kwamba alitenda kosa hilo Januari 31, 2013 mtaani Kabiria eneo la Dagoreti jijini Nairobi.

Kwenye ushahidi wake, mwanamke huyo alieleza mahakama kwamba, mshtakiwa alimvizia kwa njia na kumpiga kabla ya kumsukuma hadi nyumbani kwake ambapo alimbaka. Alidai kwamba mshtakiwa alimtisha kwa kisu ambacho pia alitumia kumtisha jirani aliyeenda kumuokoa.

“Alimweleza jirani huyo kwamba nilikuwa mpenzi wake na hakufaa kuingilia. Jirani huyo aliondoka alipogundua kwamba alikuwa na kisu,” alisema mwanamke huyo.

Angweny alikanusha madai hayo akisema alisingiziwa makosa alipotofautiana na mwanamke huyo.

Akimhukumu kwa kosa la kupiga na kujeruhi, hakimu alisema kulingana na ushahidi uliotolewa kortini, ilikuwa wazi kwamba mshtakiwa alikuwa amepanga kumdhuru mlalamishi.

You can share this post!

Wabunge walia kuhangaishwa mitandaoni

Mashine hizi zinatupotezea hamu ya uroda, wakulima wa chai...

adminleo