• Nairobi
  • Last Updated April 18th, 2024 9:15 PM
Mke wa mwalimu aliyeuawa kukaa seli

Mke wa mwalimu aliyeuawa kukaa seli

Na NDUNGU GACHANE

MKE wa mwalimu Mkuu wa Shule ya Upili ambaye mwili wake ulipatikana Jumapili ukiwa umewekwa katika buti ya gari Jumatatu alifikishwa mahakamani pamoja na mshukiwa mwingine wa kiume.

Hata hivyo, Alice Mugechi na Samuel Harrison Gitu hawakujibu mashtaka katika mahakama ya Murang’a, baada ya upande wa mashtaka kuomba muda zaidi wa kuwachunguza.

Mwili wa Bw Samuel Mbogo uligunduliwa ukiwa kwenye buti ya gari eneo la Gakurwe, kwenye barabara ya Murang’a – Kiriaini.

Afisa anayechunguza kesi hiyo Jeremiah Kazungu Ngumbao aliomba mahakama kuwapa polisi muda zaidi kukamilisha uchunguzi, kabla ya kuwafungulia rasmi mashtaka washukiwa hao.

“Naomba mahakama kutupa siku 14 zaidi ili tuweze kukamilisha uchunguzi kabla ya kuwafungulia washukiwa mashtaka kuhusiana na mauaji haya,” afisa huyo akaambia mahakama.

Lakini washukiwa walipinga ombi hilo huku wakitaka mahakama kuwaachilia huru na wakamatwe tena polisi watakapokamilisha uchunguzi.

“Hakuna mtu nyumbani wa kutunza ng’ombe na mifugo wengine. Sikupata wakati wa kufunga mlango wangu nilipokamatwa. Kadhalika, naomba nipewe muda wa kuandaa mazishi ya mume wangu mpendwa.

Polisi wako huru kunikamata tena watakapokamilisha uchunguzi wao,” akasema Mugechi. Gitu aliambia mahakama kuwa yuko tayari kukamatwa tena polisi watakapokamilisha uchunguzi wao.

“Kwa sababu polisi hawajapata ushahidi wa kunihusisha na mauaji hayo, hawafai kuendelea kunizuia. Wanikamate watakapokamilisha uchunguzi wao,” akasema mshukiwa huyo.

Lakini, Hakimu Mkuu, Bi Margaret Wachira alikataa maombi ya washukiwa akisema kuwaachilia huru kutatatiza uchunguzi.

“Nimekubaliana na ombi la upande wa mashtaka. Hivyo naruhusu afisa wa uchunguzi kuzuilia washukiwa kwa siku 14,” akasema Bi Wachira.
Kesi hiyo itatajwa Mei 28.

Mshukiwa wa kiume anadaiwa kuwa mpenzi wa mke wa mwendazake.

Kulingana na afisa mkuu wa Idara ya Upelelezi wa Murang’a Kaskazini, Bw Japheth Maingi, viatu alivyokuwa amevaa Gitu vilipatikana na damu alipokamatwa. Viatu hivyo vinadaiwa kuwa vya mwalimu mkuu aliyeuawa.

“Tulipomshika Gitu alikuwa na damu katika viatu na nguo zake na tunaamini amehusika na mauaji,” akasema afisa huyo.

You can share this post!

ODM yajitosa kwa kashfa ya Sh9 bilioni NYS

Majaji wakuu Afrika Mashariki waungana kuimarisha haki

adminleo