• Nairobi
  • Last Updated April 23rd, 2024 9:40 PM
Simbas kujaribu kupiga Cranes nyumbani

Simbas kujaribu kupiga Cranes nyumbani

Na GEOFFREY ANENE

TIMU ya taifa ya raga ya wachezaji 15 kila upande ya Kenya almaarufu Simbas, itaondoka nchini Alhamisi alasiri kuelekea Uganda kwa mechi ya mkondo wa kwanza ya shindano la Elgon Cup.

Kocha kutoka New Zealand,  Ian Snook amejumuisha wachezaji watano wapya kikosini. Wachezaji hao ni Patrick Ouko kutoka klabu ya Homeboyz, Joseph Odero (Kabras Sugar), Malcom Onsando (Kenya Harlequins), Andrew Chogo (Kabras Sugar) na Xavier Kipng’etich (Impala Saracens).

Katika hafla ya kuzindua kikosi cha wachezaji 23 watakaopeperusha bendera ya Kenya uwanjani Legends jijini Kampala hapo Jumamosi, Snook amesema Simbas imeimarika, ingawa akakiri kwamba bado kuna kazi kubwa ya kufanywa kabla ya timu kuwa fiti kabisa.

Simbas imekuwa mazoezini wiki sita pamoja na kufanya mazoezi na wanajeshi kutoka Uingereza (British Army) mjini Nanyuki. “Hii ndiyo timu nzuri tuko nayo wakati huu nchini,” Snook amesema na kufichua kwamba Kenya itakosa huduma za nahodha Wilson K’Opondo na Joshua Chisanga.

“K’Opondo anauguza jeraha naye Chisanga bado ana majukumu na klabu yake nchini Poland. Watakosa ziara ya Uganda, lakini tunawatarajia kabla ya kambi ya mazoezi nchini Afrika Kusini,” alifichua.

Meneja wa Simbas, Wangila Simiyu alisema timu ya Kenya itatafuta kupiga Uganda kwao, ingawa akakiri Cranes si wachache katika ardhi yao. Aliongeza kwamba makocha wapya kutoka New Zealand wameleta mabadiliko makubwa kikosini hasa katika idara ya mazoezi na anaamini mbinu zao mpya zitasaidia Kenya kupambana na wapinzani.

Aidha, Mkurugenzi wa timu za taifa za raga nchini, Raymond Olendo amesema Simbas pamoja na timu ya taifa ya raga ya wachezaji saba kila upande ya wanawake Kenya Lionesses zimepokea tiketi za ndege kutoka kwa serikali kusafiri nchini Uganda na Botswana, mtawalia.

Hata hivyo, Olendo alikiri Shirikisho la Raga la Kenya (KRU) bado linasubiri fedha za kufanikisha mahitaji ya timu hizo kama chakula na malazi. Simbas inahitaji Sh2 milioni nchini Uganda na Sh8 milioni katika kambi ya mazoezi nchini Afrika Kusini.

Inajiandaa kwa mechi za kufuzu kushiriki Kombe la Dunia nchini Japan mwaka 2019. Kombe la Afrika la Dhahabu (Gold Cup) mwaka 2018 litatumika kuchagua timu itakayowakilisha Afrika nchini Japan.

Gold Cup itakutanisha Kenya, Morocco, Uganda, Tunisia, Zimbabwe na mabingwa watetezi Namibia. Lionesses itakuwa jijini Gaborone nchini Botswana wikendi hii ya Mei 25-26 kuwania ubingwa wa Afrika.

Kikosi cha Kenya Simbas:

Wachezaji

Patrick Ouko*(Homeboyz), Philip Ikambili (Homeboyz), Joseph Odero* (Kabras), Malcolm Onsando* (Kenya Harlequins), Oliver Mang’eni (KCB), George Nyambua (Kabras), Elkeans Musonye (Strathmore), Tony Onyango (Homeboyz), Martin Owilah (KCB), Samson Onsomu (Impala), Isaac Adimo (Kenya Harlequins), Leo Seje (Impala), Peter Kilonzo (KCB), Darwin Mukidza, Jacob Ojee (KCB), Peter Karia (KCB), Vincent Mose (Impala), Curtis Lilako (KCB), Andrew Chogo* (Kabras), Davis Chenge (KCB), Xavier Kipng’etich Bett* (Impala), Biko Adema (Nondies) na Oscar Simiyu (KCB).

*Mbioni kuchezea Kenya kwa mara ya kwanza kabisa

Benchi la kiufundi:

Ian Snook (Kocha Mkuu), Murray Roulston (Kocha msaidizi), Dominique Habimana (Kocha wa safu ya mbele), Richard Ochieng (kocha wa mazoezi ya viungo), Christopher Makachia (daktari wa timu), Simiyu Wangila (meneja wa timu)

Ratiba ya Simbas mwaka 2018:

Mei 26 – Uganda vs. Kenya (Elgon Cup, Kampala)

Juni 23 – Morocco vs. Kenya (Africa Gold Cup, Casablanca)

Juni 30 – Kenya vs. Zimbabwe (Africa Gold Cup, Nairobi)

Julai 7 – Kenya vs. Uganda (Africa Gold Cup, Nairobi)

Agosti 11 – Kenya vs. Tunisia (Africa Gold Cup, Nairobi)

Agosti 18 – Namibia vs. Kenya (Africa Gold Cup, Windhoek)

You can share this post!

KRA yazuilia watu 21 wa kigeni waliotwaa magari kutoka kwa...

KRA na NBK kuwapa vijana mafunzo ya ushuru na uwekezaji

adminleo