• Nairobi
  • Last Updated April 19th, 2024 8:55 PM
Uhuru alitaka kunitupa ndani – Raila

Uhuru alitaka kunitupa ndani – Raila

KITAVI MUTUA na WYCLIFFE MUIA

KINARA wa ODM, Raila Odinga Jumanne alifichua kuwa Rais Uhuru Kenyatta alikuwa amepanga kumkamata na kumshtaki kwa uhaini baada ya kujiapisha kama ‘rais wa wananchi’ mnamo Januari 30 mwaka huu.

“Baada ya kuapishwa, niligundua kuwa Uhuru alikuwa anashinikizwa na wandani wake anikamate na akashawishika. Lakini baada ya kubaini athari za hatua hiyo akabadili mpango huo,” alisema Bw Odinga akiwa Kitui.

Kwa upande wake, Bw Odinga alikuwa na shinikizo kali kutoka kwa wandani wake wenye misimamo mikali waliomtaka aingie Ikulu kwa mabavu, awashauri wafuasi wake kuacha kulipa ushuru kwa serikali na pia wachome picha za Rais Kenyatta.

Akisimulia kwa mara ya kwanza matukio yaliyopelekea yeye na Rais Kenyatta kuafikia mwafaka wa maridhiano hapo Machi 9, Bw Odinga alielezea jinsi yeye na Rais Kenyatta walivyojipata katika hali ngumu ya kisiasa hasa kutoka kwa wandani wao wenye misimamo mikali, hali iliyowalazimu kuamua kibinafsi kuchukua hatua za kuepusha Kenya kutumbukia katika ghasia za kikabila na kisiasa.

Akizungumza baada ya kufungua hoteli ya kifahari inayomilikiwa na msomi wa masuala ya sheria Prof Makau Mutua katika Kaunti ya Kitui, Bw Odinga alisema kama hawangeshirikiana Kenya sasa ingekuwa kama Syria ama Yemen.

Alisema wafuasi wake walikuwa wakimshinikiza aingie Ikulu kwa nguvu baada ya kujiapisha kuwa ‘rais wa wananchi’ huku wafuasi wa Rais Kenyatta nao wakimpa presha amkamate na kumfungulia mashtaka ya uhaini, ambayo hukumu yake ni kifo kwa kunyongwa.

“Tayari wafuasi wangu walikuwa wameanza kung’oa picha za Rais Kenyatta kutoka kwenye majengo na biashara zao huku wengine wakitishia kutolipa ushuru.

Wafuasi wetu walikuwa tayari kuanza kutukubalia tuchukue ushuru kutoka kwao,” alisema Bw Odinga katika hafla aliyoandamana na mkewe Aida na kuhudhuriwa na kinara wa Wiper Kalonzo Musyoka, Gavana Charity Ngilu wa Kitui na mwenzake wa Makueni, Kivutha Kibwana.

Bw Odinga alifichua kuwa mwanzoni Rais Kenyatta alikuwa amekubali kumkamata na kumfikisha kortini lakini akabadili msimamo baada ya kutathmini athari za hatua hiyo.

“Tulikuwa tumekubaliana tuanze kukusanya ushuru katika ngome zetu lakini baada ya kufikiria zaidi nikaona kuwa kama taifa tungetumbukia shimo sawa na nchi za Yemen na Syria. Rais naye aliacha mpango wa kunikamata na tukaamua kushirikiana,” alisema Bw Odinga.

Alidokeza kabla ya mwafaka, alikuwa kwenye njia-panda kuhusu kuwaridhisha wandani wake, ambao walikuwa wamekasirishwa na ukosefu wa uchaguzi huru na wa haki, ama kufanya kilicho bora kwa taifa zima kwa jumla.

“Iwapo ningetii mwito wa wafuasi wangu waliokuwa na hasira nyingi na kuwaruhusu kuandamana kote nchini, Serikali ya Jubilee ingewakabili kwa dhuluma kali na hili lingepeleka nchi kwenye njia hatari sana,” akasema.

Alisema hivi karibuni Wakenya wataanza kufurahia matunda ya mwafaka mara jopo lililobuniwa kutathmini ajenda tisa za maafikiano litakapoanza shughuli zake.

Aliongeza kuwa baada ya miaka minane ya utawala chini ya Katiba mpya, huu ni wakati mwafaka wa kuichunguza upya na kuziba mianya ambayo itapatikana.

Bw Odinga alimkosoa Naibu Rais William Ruto kwa kudai kuwa alifahamu kuhusu mazungumzo yake na Rais Kenyatta kabla ya kusalimiana nje ya Jumba la Harambee mnamo Machi 9, mwaka huu.

 

Ruto, Kalonzo walikuwa gizani

Bw Odinga alisema walikubaliana na Rais Kenyatta wasimhusishe Bw Ruto katika mazungumzo yao. “Nilimwambia Uhuru kuwa sitaki watu wanaopiga siasa za 2022 wahusishwe katika muafaka wetu. Rais aliahidi kuwa hatahusisha Ruto naye akanitaka pia ni nisimwambie Kalonzo,” alisema Bw Odinga.

Kauli ya Bw Odinga inatofautiana na msimamo wa Bw Ruto kuwa Rais Kenyatta alimshauri kabla ya kufanya muafaka na Waziri huyo Mkuu wa zamani.

Bw Odinga aliwataka wafuasi wake Ukambani kuunga mkono muafaka wake na Rais Kenyatta akisema utawafikisha ‘Canaan’ baada ya kutekelezwa kikamilifu.

Kwa upande wake, Bw Musyoka alimtaka Odinga kutumia muafaka wake na rais kuhakikisha kuwa viongozi wa upinzani wameondolewa mashtaka waliyofunguliwa wakati wa uchaguzi.

“Mheshimiwa Johnstone Muthama angekuwa hapa leo iwapo hangekuwa anakabiliwa na kesi yake wakati wa uchaguzi. Tulitarajia muafaka ungeondolea mbali kesi hizo,” alisema Musyoka.

Bw Odinga alimsifu Prof Mutua na kutaka jamii ya Wakamba kuhakikisha imefaidika kutoka kwa hekima yake ya uongozi.

“Nilipokuwa naja huku nilimfahamisha Rais Kenyatta na akanituma niambie Mutua aache kuwa mkosoaji sugu kwake,”alisema Bw Odinga.

You can share this post!

Huenda Rotich na Bett wakashtakiwa kuhusu sukari

Si miti tu, ukataji nyasi pia ni haramu, serikali yafafanua

adminleo