• Nairobi
  • Last Updated April 24th, 2024 10:08 PM
WASONGA: TSC, walimu waelewane kukomesha mgomo shuleni

WASONGA: TSC, walimu waelewane kukomesha mgomo shuleni

Na CHARLES WASONGA

SHULE zilifungwa wiki iliyopita baada ya kukamilika kwa muhula wa pili ulioshuhudia visa vingi vya utovu wa nidhamu, hasa katika shule za upili.

Shule kadhaa zilifungwa, kwa muda, baada ya wanafunzi kuteketeza mabweni yao, kama hatua ya kutuliza hali. Hii ina maana mkondo wa masomo katika shule uliathirika kiasi kwamba baadhi ya walimu hawakuweza kukamilisha silabasi inavyopasa.

Kwa hivyo, muhula wa tatu utakapoanza mapema Septemba, walimu watakuwa mbioni kuwaanda watahiniwa kwa mitihani ya kitaifa ya darasa la nane (KCPE) na kidato cha nne (KCSE) itakayoanza mwishoni mwa Oktoba.

Hii ndio maana ni muhimu kwa serikali, Tume ya Kuajiri Walimu Nchini (TSC) na vyama vya kutetea masilahi ya walimu (Knut na Kuppet) kuzungumza na kuelewana kwa lengo la kukomesha mgomo ambao umeitishwa mapema mwezi ujao.

Walimu, kupitia vyama hivyo, wametangaza kuwa watagoma kuanzia Septemba mosi ikiwa TSC haitatimiza matakwa kadhaa waliyowasilisha, kama vile, kusitishwa kwa uhamisho wa walimu na utathmini wa utendakazi wao.

Vile vile, walimu wanataka wenzao waliopanda ngazi kimasomo wapandishwe vyeo, pendekezo ambalo TSC imepinga.

Mapema mwaka huu vigogo wa kisiasa nchini, Rais Uhuru Kenyatta na Raila Odinga, walionyesha mfano mzuri wa kumaliza tofauti kati yao kwa kuketi katika meza ya mazungumzo, hatua iliyomaliza joto la kisiasa nchini.

Wawili hao waliweka kando tofauti zao za kisiasa kwa manufaa ya Wakenya milioni 45 ambao waliathirika pakubwa kufuatia ghasia zilizoshuhudiwa maeneo kadha nchini.

Sasa taifa linavuna matunda ya muafaka kati ya Uhuru na Odinga kwani sekta mbalimbali za kiuchumi, mathalan utalii, zimeanza kuimaika huku vita dhidi ya ufisadi vikiendeshwa kwa kasi.

Kwa mantiki hiyo hiyo, TSC inafaa kuzungumza na vingozi wa Knut na Kuppet ili kuzuia mgomo wa walimu ambao huenda ukatatiza masomo na mitihani ya KCPE na KSCE.

Endapo walimu watatekeleza tishio lao bila shaka watakaoathirika moja kwa moja ni watahiniwa kwani maandalizi yao yatavurugika. Matokeo ya hali hii ni kwamba wanafunzi wataandikisha matokeo duni hali ambayo, bila shaka, itaathiri mustakabali wao.

Aidha, huenda ratiba ya mitihani hiyo ikabadilishwa, hatua ambayo itaigharimu serikali na wazazi fedha zaidi.

Kwa hivyo, Wizara ya Leba inapasa kuingilia kati vuta nikuvute hii katika ya TSC na walimu kwa lengo la kuzima mgomo.

Waziri Ukur Yattani anafaa kuitisha mkutano wa pamoja ya viongozi wa Knut na Kuppet na maafisa wa TSC ili kutatua tofauti kati yao kwa manufaa ya wanafunzi.

Wahusika katika suala hili waige mfano wa Rais Kenyatta na Odinga ili kuleta utulivu katika sekta ya elimu.

[email protected]

You can share this post!

OBARA: Twahitaji muujiza wa pili ili mwafaka ufanikiwe

Nusra afutwe kazi kwa kuonja mlo wa mdosi

adminleo