• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 3:25 PM
Binti gaidi mwenye umri mdogo zaidi duniani atupwa jela maisha

Binti gaidi mwenye umri mdogo zaidi duniani atupwa jela maisha

Na MASHIRIKA na CHARLES WASONGA

LONDON, Uingereza

GAIDI wa kike mwenye umri mdogo zaidi duniani, ambaye ni mwanachama wa kundi moja la kigaidi nchini Uingereza Ijumaa alihukumiwa kifungo cha maisha kwa kupanga mashambilio London, mnamo 2017.

Polisi walisema kuwa Safaa Boular, 18,  alishirikiana na mamake pamoja na dadake kutekeleza uhalifu huo baada ya juhudi zake za kujiunga na kundi la kigaidi la Islamic State (IS) nchini Syria kutibuliwa.

“Wanawake hao watatu walijawa na chuki na itikadi mbaya na walikuwa wanapanga kutelekeza shambulio la kigaidi,” Naibu Kamishna wa polisi Dean Haydon, ambaye pia ni mshirikishi wa kikosi cha kupambana na ugaidi, alisema.

“Kama wangefauli, wangewaua watu wengi na wengine wengi wakijeruhiwa,” akaongeza kwenye taarifa kwa vyombo vya habari.

Maafisa wa upelelezi walinakili mawasiliano ya simu kati ya watatu hao ambapo ilibainika kuwa wapanga kuandaa “karamu” baada ya kufanikisha mipango yao.

Wapelelezi hao waliwafuata  huku wakizunguka katika barabara za London mnamo Aprili 2017, katika kile maafisa wa polisi wanaamini ilikuwa ni ziara yao ya kutambua vituo ambavyo wangeshambulia.

Siku iliyofuata walienda kwa duka moja la Supermarket katika eneo la Wandsworth, kusini magharibi mwa London ambapo walinunua paketi yenye visu vya jikoni.

Miezi miwili baadaye, dadake Boular, Rizlaine Boular, 22, alifungwa maisha pamoja na kifungo kisichoweza kukatiwa rufaa cha miaka 16 katika jela Old Bailey.

Mamake, Dina Dich, 44, alipewa kifungu cha miaka 11 na miezi tisa gerezani, adhabu ambayo hangeweza kukata rufaa dhidi yake. Hii ni kando na kifungo cha maisha.

You can share this post!

Lucy Wangui agunduliwa kuwa mtumizi sugu wa pufya

Kocha asifu vijana wake kuandaa gozi kama alivyowaagiza

adminleo