• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 1:29 PM
TAHARIRI: Polisi watumikie wananchi wote

TAHARIRI: Polisi watumikie wananchi wote

NA MHARIRI

TUKIO la Jumatatu ambapo maafisa wa polisi walifyatua risasi mazishini na kujeruhi watu kadhaa lazima lishutumiwe.

Maafisa hao walijeruhi watu kwa risasi, wakiwemo polisi wenzao ambao ni walinzi wa wabunge, wakati wa mazishi ya dereva wa mbunge wa Likuyani, Dkt Enock Kibunguchy.

Mazishi ya marehemu Douglas Wakachi yalikumbwa na fujo, huku ikibainika kuwa polisi hawajapiga hatua yoyote kumtia mbaroni hata mshukiwa mmoja.

Dereva huyo aliuawa usiku wa Jumapili, Agosti 12 akiwa ndani ya gari la Dkt Kibunguchy, aliyekuwa ameingia ndani ya Highway Motel eneo la Soy.

Japokuwa Naibu kamanda msimamizi wa polisi eneo la Magharibi, Bw Leonard Omollo alisema maafisa wake walianzisha msako wa kuwakamata washukiwa, inangia wiki ya tatu bila ya kuwepo hata fununu kuhusu watu hao.

Hali hii inaibua maswali kuhusu utendakazi wa maafisa waliokabidhiwa jukumu la kulinda maisha ya watu na mali zao. Inaonekana ni kama polisi hutafuta njia za mkato za kusuluhisha mambo, badala aya kufuata sheria inavyosema.

Hali hii ya kutotaka kufuatilia matukio pia inashuhudiwa katika kaunti ya Kericho, ambapo maafisa wa kituo cha Kericho wanakashifiwa kuwa wanajaribu kuficha ukweli kuhusu kilichosababisha kifo cha manafunzi wa mwaka wa tatu katika Chuo Kikuu cha Kabarak.

Wazazi wa kijana Edwin Kipkemoi wanadai kuwa polisi wamekataa kushirikiana nao ili kujua ukweli kuhusu kilichomuua. Wanalalama kwamba hawajaruhusiwa kuona ripoti iliyopigwa humo.

Matukio haya yanaibua maswali mengi kuhusu kujitolea kwa polisi kuitikia mwito wao wa Utumishi kwa Wote. Je, polisi sasa wamegeuka kuwa wa kuwatumikia watu wakubwa pekee serikalini? Ni kwa nini suala linapomhusu mtu asiyekuwa na ushawishi huwa halipewi uzito wowote?

Kuna maagizo maalum kwa polisi kwamba wawe wakipuuza malalamishi ya wasiokuwa wanasiasa au watu wasio na pesa? Ikiwa hakuna maagizo, ni kwa sababu gani maafisa hawa wanaruhusiwa kufanya kazi kwa kutumia mwongozo wanaojitungia?

Kuna haja ya kutazama upya utendakazi wa maafisa wa polisi. Hata ikibidi kurejelewa kwa upigaji msasa, ni lazima mwananchi anayelipa ushuru wanaolipwa maafisa hao, apewe hadhi yake kama mwajiri nambari moja wa watumishi wa umma.

You can share this post!

NGILA: Kampuni ziheshimu taarifa za siri za Wakenya

Vilio vya demu vyakosa kuzima harusi kanisani

adminleo