• Nairobi
  • Last Updated April 25th, 2024 5:29 PM
Ruto na Waiguru wachemka kutajwa kuwa wafisadi zaidi

Ruto na Waiguru wachemka kutajwa kuwa wafisadi zaidi

Na PETER MBURU

NAIBU Rais William Ruto na Gavana wa Kirinyaga Bi Anne Waiguru wamekemea vikali matokeo ya kura ya maoni ya Ipsos Synovate ambayo yaliwaorodhesha kama maafisa wa umma wafisadi zaidi nchini.

Matokeo ya kura hiyo ya maoni yaliashiria kuwa Bw Ruto na Bi Waiguru ndio wanashikilia nambari moja na mbili mtawalia kwa ufisadi, kulingana na maoni ya wakenya.

Kati ya wakenya 2,016 waliohojiwa  kote nchini, zaidi ya 660 walisema kuwa wanadhani Bw Ruto ndiye mfisadi zaidi nchini, huku angalau 624 wakisema Bi Waiguru ndiye wa pili kwa madoa ya ufisadi.

Lakini viongozi hao wawili hawakuchukulia suala hilo kwa wepesi, Bi Waiguru akitishia kuishtaki kampuni ya Ipsos kwa kumchafulia jina, nao wandani wa naibu wa rais wakipuuzilia matokeo hayo kuwa ya kumharibia juhudi zake za kuwa rais ifikapo 2022.

“Ipsos inatumiwa na wanasiasa kunichafulia jina kwa kuwa wanahofia kuhusu 2022. Wameona kuna maendeleo Kaunti ya Kirinyaga na wamekasirika,” Bi Waiguru akasema Jumatano, baada ya matokeo hayo kutolewa.

Mkuu wa mawasiliano katika ofisi ya naibu wa rais pia alishikilia kuwa utafiti huo ulifadhiliwa na watu walio na nia ya kujenga dhana kuwa Bw Ruto ni mfisadi miongoni mwa wakenya ili kumharibia juhudi za kufika ikulu.

“Matokeo hayo ni hila za waliofeli kisiasa, wawezaje kupima dhana?” akauliza Bw Mugonyi.

Lakini akitoa matokeo hayo, mtafiti mkuu wa Ipsos Prof Tom Wolf alisema mtu hawezi kuwashtaki kwani matokeo yao yaliakisi wanavyofikiria wakenya, akisema hayo ni maoni tu ila si hukumu kwa waliotajwa.

“Kazi ya kudhibitisha ikiwa mtu aliyetajwa ni mfisadi au la ni ya idara nyingine kama mahakama, letu ni kusema wanavyodhani wakenya tu,” akasema Prof Wolf.

You can share this post!

Babu Owino na wenzake watisha kuandamana Kampala kumnusuru...

Bei ya sukari kushuka

adminleo