• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 11:42 PM
Nitarudi Kenya Septemba 4, mpende msipende – Miguna

Nitarudi Kenya Septemba 4, mpende msipende – Miguna

Na BENSON MATHEKA

WAKILI mbishi Dkt Miguna Miguna aliyefurusha nchini mara mbili baada ya kuongoza hafla ya kumuapisha Raila Odinga kuwa “rais wa wananchi”, amesema kwamba atarejea nchini baada ya Septemba 4, 2018.

Kupitia ujumbe wa Twitter Alhamisi, Dkt Miguna anayeishi Canada, alitangaza kuwa hakuna kitakachomzuia kurejea Kenya licha ya serikali kumpokonya paspoti yake ya Kenya na kuiharibu.

“Nitarudi baada ya Septemba 4, shime,” aliandika kwenye Twitter.

Hili litakuwa jaribio la tatu la wakili huyo kurudi Kenya tangu Februari alipotimuliwa Kenya mara ya kwanza.

Mnamo Machi 16, Dkt Miguna alitangaza kuwa angerejea Kenya lakini hakufanya hivyo.

Alifurushwa Kenya Februari 6 siku sita baada ya kumuapisha Bw Odinga katika bustani ya Uhuru Park. Serikali ilidai kuwa alipoteza uraia wake wa Kenya na kwamba alikuwa nchini kinyume cha sheria.

Wakili huyo amekuwa akishikilia kuwa hajawahi kukana uraia wake wa Kenya, nchi aliyozaliwa na kwamba serikali ilikiuka agizo la mahakama kwamba arejeshewe paspoti yake na kuruhusiwa kuingia nchini.

Waziri wa usalama Fred Matiang’i alisema Miguna ambaye ana uraia wa Canada anapaswa kuomba upya uraia wake ili apate paspoti ya Kenya na kuruhisiwa kuingia Kenya.

Kulingana na serikali, Bw Miguna alipata paspoti iliyotwaliwa kinyume cha sheria.

Wakili Miguna amekataa kujaza fomu kuomba uraia wa Kenya akisema mtu hawezi kupoteza uraia wake wa kuzaliwa.

Amekuwa akikosoa muafaka kati ya Rais Kenyatta na Rais Kenyatta anaotaja kama usioweza kutatua shida zinazowatatiza Wakenya.

Kupitia jumbe za Twitter, Miguna amekuwa akidai kwamba Bw Odinga aliwasaliti wafuasi wake kwa kukubali kushirikiana na serikali.

Bw Odinga amenukuliwa akisema kwamba wakili huyo ni mtu asiyeweza kusaidiwa kwa sababu ya msimamo wake mkali.

Kwenye ujumbe wa kutangaza kurejea nchini mwezi ujao, Miguna alimlaumu Raila na Rais Kenyatta kwa masaibu yake.

“Mliharibu paspoti yangu ya Kenya na nyumba yangu, mkanikamata na kunitesa kabla ya kunifurusha, mnaweza kuandika haya kwa wino usiofutika: Nitarejea baada ya Septemba 4,” alisema.

You can share this post!

Aliyeanika picha kujitapa anavyonajisi watoto anyakwa

IPSOS: Wakenya wamsifu Kalonzo kama asiye na doa la ufisadi

adminleo