• Nairobi
  • Last Updated April 20th, 2024 3:03 PM
DIMBA: ‘Big Mo’ Kean ametajwa kama kizazi kipya cha Azzuri

DIMBA: ‘Big Mo’ Kean ametajwa kama kizazi kipya cha Azzuri

Na GEOFFREY ANENE

BIOTY Moise Kean ni mmoja wa wanasoka makinda wanaovuma kwenye Ligi Kuu nchini Ufaransa.

Mshambuliaji huyo wa kati mwenye nguvu na kasi anachezea klabu ya Paris Saint-Germain. Anaaminiwa kuwa mmoja wa wachezaji nchi ya Italia itategemea kuinua soka yake tena.

Italia imepitia changamoto kadhaa katika soka yake ikiwemo Azzuri kukosa Kombe la Dunia kwa mara ya kwanza katika kipindi cha miaka 60 mwaka 2018 kutokana na talanta kupungua.

Moise yuko katika kizazi kipya cha talanta kinachotarajiwa kurejeshea Italia sifa ya kuwa miamba wa soka ambayo walikuwa wamejizolea kwa miaka nyingi.

Mwanasoka huyo aliye na asili ya Ivory Coast, anachezea PSG kwa mkopo kutoka kwa Everton inayoshiriki Ligi Kuu Uingereza.

Mamaye Isabelle Dehe na babaye Biorou Jean Kean walihamia kaskazini mwa Italia katika mji wa mjini Vercelli kutoka nchini Ivory Coast kutafuta maisha mazuri.

Walimpata Moise mnamo Februari 28 mwaka 2000. Ripoti zinasema alizaliwa kimiujiza baada ya Isabelle kuambiwa na madaktari kuwa hawezi kupata watoto zaidi.

‘Big Mo’ anavyofahamika sasa kwa jina la utani, alilelewa na mzazi mmoja: Isabelle. Wazazi wake walitengana akiwa na umri wa miaka minne. Babake alirejea Ivory Coast na mamake kulazimika kuwa yaya ili kulea familia ya watoto wawili nchini Italia.

Moise alianza uchezaji wake katika soka ya mtaani baada ya familia hiyo kuhamia mjini Asti. Alipendezwa sana na soka ya mshambuliaji wa Nigeria Obafemi Martins ambaye alikuwa mali ya Inter Milan wakati huo.

Alipiga hatua kwa sababu ya kipa wa zamani wa Torino, Renato Biasi ambaye alitambua talanta yake na kumshika mkono katika safari yake. Biasi alimuingiza katika akademia ya Asti mwaka 2007 kabla ya kumwasilisha Torino mwaka uo huo.

Moise alikuwa na Torino hadi 2010 aliponyakuliwa na miamba Juventus. Alitumia mazingira mapya kuimarisha soka yake akijiunga na timu ya watu wazima ya Juve baada ya miaka sita, ikiwemo kuifungia mabao 24 katika mechi 25 msimu 2015-2016.

Alianza soka ya malipo katika timu ya Juve mnamo Novemba 19, 2016 akitumiwa dhidi ya Pescara kama mchezaji wa akiba katika nafasi ya gunge Mario Mandzukic katika ushindi wa mabao 3-0.

Alikuwa na umri wa miaka 16, miezi minane na siku 23 wakati wa mchuano huo wa Ligi Kuu ya Serie A; umri ambao ulimfanya kuwa mchezaji wa kwanza aliyezaliwa miaka ya 2000 kushiriki mojawapo ya ligi nne kubwa barani Ulaya.

Aliandikisha rekodi nyingine kama hiyo aliposhiriki Klabu Bingwa Ulaya siku chache baadaye timu ya Juve ikichapa Sevilla 3-1 nchini Uhispania.

Katika mechi ya mwisho msimu huo, Moise pia aliweka rekodi ya kuwa mfungaji aliyezaliwa miaka ya 2000 kupachika bao katika mojawapo ya ligi tano kubwa barani Ulaya, timu yake ya Juve ikilaza Bologna 2-1 ugenini.

Licha ya kuendelea kuimarika, Moise alipelekwa Verona kwa mkopo msimu uliofuata kabla ya kurejea Juventus kwa msimu 2018-2019 na kisha kuuziwa Everton kwa Sh3.7 bilioni kwa kandarasi ya miaka mitano.

Katika msimu wake wa mwisho na Juve, Moise alibaguliwa kwa rangi na mashabiki wa Cagliari na kutetewa na nyota Raheem Sterling, Mario Balotelli na Paul Pogba baada ya Mwitaliano mwenzake Leonardo Bonucci kudai kinda huyo alichangia katika kubaguliwa kwake.

Hakufanya vizuri katika mechi 33 alizopewa uwanjani Goodison Park katika mashindano yote msimu 2019-2020 na kuelekea PSG kwa mkopo msimu huu.

Amejitokeza kuwa mojawapo wa wachezaji wazuri kwenye Ligue 1. Alianza msimu huu Everton kabla ya kuelekea PSG mnamo Oktoba 4, 2020.

Moise, ambaye aliwahi kumezewa mate na Manchester City na Arsenal, yuko katika vuta-nikuvute na PSG inayotaka aendelea kuwa naye huku Juve ikitaka kumnunua tena. Bei yake sokoni ni Sh4.7 bilioni.

Moise amelinganishwa kimchezo na Balotelli, ambaye pia wanatumia wakala mmoja Mino Raiola.

Kinda huyo anatoka katika familia ya wanasoka. Kakake mkubwa Giovanni Kean Dosse, 27, ni mshambuliaji wa kati wa US Termoli 1920. Pia ana binamu wawili wanaosakata soka ya kulipwa. Mshambuliaji wa kati Massimo Goh, 21, anayechezea Marignanese Calcio katika moja ya ligi ndogo za nchini Italia. Kisha beki Abdoulaye Bamba, 30, wa timu ya Angers inayoshiriki Ligi Kuu ya Ufaransa (Ligue 1).

You can share this post!

WARUI: Hatua ya dharura yahitajika kuzima utovu wa nidhamu...

Benzema afunga mabao mawili na kupaisha Real Madrid hadi...