• Nairobi
  • Last Updated April 23rd, 2024 4:25 PM
Kifafa hakijamzuia kutimiza ndoto yake

Kifafa hakijamzuia kutimiza ndoto yake

Na PAULINE ONGAJI

Licha ya changamoto anazokumbana nazo maishani kama mwathiriwa wa maradhi ya kifafa, kila siku anajizatiti kuishi maisha ya kawaida.

Huo ni uhalisi wa Bi Harriet Nyokabi, 25, mkazi wa mtaa wa Githurai 45, Kaunti ya Nairobi.

Bi Nyokabi ameishi na maradhi haya tokea utotoni, suala ambalo limeathiri maisha yake ya kaiwada.

Amekuwa akikabiliana na kifafa tangu awe na miaka minne baada ya kugongwa na gari. Ni tukio lililomlazimu kulazwa katika chumba cha watu mahututi kwa miezi sita, kabla ya kupona na kuruhusiwa kwenda nyumbani.

Lakini huo haukuwa mwisho wa masaibu yake kwani pindi baadaye, mashambulio ya kifafa yalianza.

“Ni suala lililoathiri pia masomo yangu ambapo nililazimika kuacha shule nikiwa katika darasa la nne kwani mashambulio hayo yalizidi,” aeleza.

Ni suala lililowakosesha amani sio tu wanafunzi, bali pia walimu wake huku jitihada za mamake kumtafutia shule zikigonga mwamba kila alipoeleza kuhusu hali yake.

Haya yote ni kando na matatizo ambayo amekuwa akikumbana nayo kama mwathiriwa wa maradhi ya kifafa ambapo analazimika kumeza tembe saba kila siku ili kjudhibiti hali hii.

Isitoshe, kila siku ni changamoto kwa mama huyu wa watoto wawili kwani anakumbwa na hatari ya kujeruhiwa kutokama na mashambulio ya kila mara, huku maisha yake yakiwa magumu hata zaidi hasa ikizingatiwa kwamba mkono wake wa kushoto umepooza kidogo.

Lakini licha ya hayo, badala ya kukaa kitako na kujionea huruma, Bi Nyokabi amejitahidi kimaisha. Kwa mfano, kwa sasa anamiliki duka la kushona nguo, kazi aliyoanzisha baada ya kupokea cherehani kutoka chuo cha mafunzo ya kiufundi ambapo alikuwa akijifunza.

“Mojawapo ya sababu zilizomfanya kujishindia mtambo huu ni bidii na ukamavu wake katika kipindi chote cha mafunzo kwani hakuwahi kosa chuoni licha ya changamoto za kiafya alizokumbana nazo,” asema Fred Kiserem, mwanzilishi wa chuo cha mafunzo ya kiufundi cha Kiserem Vocational Center.

Kumbuka alipokuwa akipokea mafunzo haya, pia alikuwa akifanya kazi ya kuchuuza matunda, ambapo alilazimika kutembea kwa kilomita kadhaa kila siku kufikishia wateja wake bidhaa hii.

Japo anakiri kwamba kwake, kila siku maisha ni kupambana, anatumai kwamba matatizo hayo hayatakuwa kizingiti katika harakati zake za kutimiza ndoto zake maishani. Ndoto yake ni kuimarisha biashara yake ya nguo na hata wakati mmoja kumiliki duka kubwa la biashara.

“Bila shaka kila siku ni changamoto, lakini watu wanapaswa kuelewa kwamba mimi binadamu kama wengine. Ningependa hadithi yangu iwe ushuhuda kwa kila mmoja anayekumbwa na hali kama yangu,” asema.

You can share this post!

DJ anayetumia miguu kuburudisha Wakenya

Montreal Impact ya Wanyama yalipiza kisasi dhidi ya Toronto