• Nairobi
  • Last Updated April 18th, 2024 9:15 PM
Maiti bila kichwa na mikono yapatikana katika shamba la mpunga

Maiti bila kichwa na mikono yapatikana katika shamba la mpunga

NA MWANGI MUIRURI

WENYEJI wa eneo la Mwea katika Kaunti ya Kirinyaga mnamo Jumanne wamepigwa na butwaa baada ya kukumbana na mwili wa mwanamume bila kichwa ukiwa umetupwa katika shamba la mpunga.

Maiti hiyo haikuwa na kichwa na mikono na wenyeji walielezea wasiwasi wao wakisema yalikuwa mauaji ya kishetani.

“Tumeona visa vya mauaji lakini hiki cha mtu kuuawa na kukatwa kichwa na mikono kinadhihirisha ukatili uliovuka mipaka,” akasema mkazi mmoja aliyesema anaitwa Bw Japhat Mureithi.

Maafisa wa polisi wa kituo cha polisi cha Kiamaciri wameitwa na kuchukua maiti hiyo ambayo bado haijatambulika.

Kamishna wa Kaunti ya Kirinyaga Bw  Nayioma Tobiko amesema kisa hicho ni cha kusikitisha na polisi tayari wamezindua uchunguzi.

“Tumefanya uchunguzi wa msingi katika eneo ambapo maiti imepatikana. Kinaonekana kuwa kisa cha mauaji na kisha maiti kusafirishwa na kutupwa mahali hapo,” akasema.

Bw Tobiko amesema kwamba uchunguzi wa kina utatekelezwa “tukianza na bidii ya kumtambua aliyeuawa, mara yake ya mwisho kuonekana akiwa hai, aliokuwa nao, akawasiliana na kina nani, akatoweka wapi na lini… hayo maswali yote ndiyo tutajibu”.

Ameongeza kuwa upasuaji wa mwili tena utatoa mwelekeo wa uchunguzi “bila kusahau kuwa bado tuko na kibarua cha kusaka kichwa na mikono ya marehemu”.

  • Tags

You can share this post!

Maanzo, Otiende Amollo kuongeza ladha kesi ya kupinga...

Lilian Mbogo aondolewa lawama ya uporaji mamilioni NYS

T L