• Nairobi
  • Last Updated April 19th, 2024 5:55 AM
‘Marehemu alifichua waliomuua kabla ya kufa’

‘Marehemu alifichua waliomuua kabla ya kufa’

Aliyekuwa diwani wa wadi ya Riruta, Nairobi, Bw Samwel Ndungu. Picha/ Maktaba

Na ERIC WAINAINA

DAKIKA chache kabla ya kufariki, Bi Lucy Njambi, mke wa aliyekuwa diwani wa wadi ya Riruta, Nairobi, aliambia watu wa familia na madaktari kwamba ni mumewe aliyepanga shambulio ambalo alichomwa mwili kwa asidi, Mahakama Kuu ilifahamishwa Jumanne.

Hii ilielezwa kwenye kesi ambapo mumewe marehemu, Samwel Ndung’u, Bi Joyce Njambi, ambaye anadaiwa kuwa mpenzi wake na Bw Wilson Mwangi, wameshtakiwa katika Mahakama Kuu ya Kiambu kwamba mnamo Januari 24 walishirikiana na watu wengine ambao hawajashtakiwa kumuua Bi Njambi, 24.

Bi Esther Nyambura, ambaye ni shangazi ya marehemu, aliambia mahakama kwamba mnamo Januari 24, baada ya mwathiriwa kupelekwa hospitali ya Kiambu Level Five na Msamaria Mwema aliyempata Kamiti Corner, familia ilipokea simu kutoka hospitali hiyo na wakakimbia huko mara moja.

Akitoa ushahidi, Bi Nyambura alisema alipofika hospitali mwendo wa saa kumi na mbili asubuhi alimpata marehemu kitandani.

“Nilimuuliza kama alinifahamu na akajibu ndio. Nilimuuliza kilichotendeka na akajibu, ‘haki ni baba Njoro’ , muulize,” Bi Nyambura aliambia mahakama.

Baada ya muda mfupi, Bi Njambi ambaye alisema alikuwa na maumivu mengi, alihamishiwa hospitali ya Kitaifa ya Kenyatta ambapo aliandamana na watu wachache wa familia akiwemo Bi Nyambura.

Katika hospitali ya Kenyatta, Bi Nyambura, ambaye mara kwa mara alishindwa kuzuia machozi kortini, alisema alimuuliza kilichotendeka na akarudia kwamba ni mumewe aliyehusika na baadaye alipoulizwa na madaktari alitoa jibu hilo hilo.

Bi Fidelis Muthoni, ambaye pia ni shangazi wa marehemu, aliambia mahakama kwamba kabla ya kisa hicho, Bi Njambi alikuwa amemweleza kwamba alihofia maisha yake kwa sababu Ndun’gu alikuwa akidai alikuwa na uhusiano kimapenzi na wanaume wengine.

Kesi inaendelea.

 

You can share this post!

Atoroka baada ya kuua mtu na kunywa damu yake

Kundi lamtetea Oparanya kwa kuhudhuria hafla ya Jubilee

adminleo