• Nairobi
  • Last Updated April 23rd, 2024 8:31 PM
Meru kuendelea kufaidi mradi wa kuboresha kilimo cha viazi

Meru kuendelea kufaidi mradi wa kuboresha kilimo cha viazi

Na SAMMY WAWERU

SERIKALI ya Kaunti ya Meru imetangaza kwamba wakulima wa eneo hilo wataendelea kupata mafunzo ya ukuzaji bora wa viazimbatata yanayotekelezwa na Uholanzi. 

Uholanzi ni kati ya mataifa wazalishaji wakuu wa viazi duniani, na imekuwa ikishirikiana na Meru kwa muda wa miaka mitatu sasa katika utoaji wa mafunzo faafu kuvizalisha.

Kulingana na Waziri wa Kilimo, Ufugaji na Samaki (CEC) kaunti hiyo Bi Caroline Kagwiria, mafunzo hayo pia yanajumuisha matumizi ya mbegu bora, mbolea na dawa.

“Zaidi ya wakulima 3, 000 wamenufaika kufikia sasa,” Bi Caroline akasema akizungumza jijini Jairobi, katika hafla iliyoleta pamoja wadauhusika katika uzalishaji wa viazimbatata nchini.

Waziri alisema mradi huo unalenga wadi ambazo ni tajika katika ukuzaji wa viazi Meru. “Umetekelezwa katika wadi ya Timau, Kisima na Kibirishia,” akasema.

Bi Caroline Kagwiria, Waziri wa Kilimo, Ufugaji na Samaki (CEC) Meru, ametangaza kwamba kaunti hiyo itatia upya saini mkataba wa makubaliano kati ya Meru na Uholanzi, mradi wa mafunzo bora ya ukuzaji wa viazi uendelee kutekelezwa…PICHA/ SAMMY WAWERU

Huku mkataba wa makubaliano ya utekelezaji wa mradi huo, kati ya Meru na serikali ya Uholanzi, ukitarajiwa kufikia kikomo mwaka ujao, Waziri Caroline alisema Gavana Kiraitu Murungi na Balozi wa Uholanzi hapa nchini Kenya, Bw Marteen Brouwer wamekubaliana kuuendeleza kipindi kingine.

“Watia upya saini ya makubaliano uendelezwe kipindi kingine cha miaka mitatu, minne au mitano,” akadokeza. Kaunti ya Nakuru na Kajiado zikiendelea kutekeleza sheria ya upakiaji wa viazi, ambapo vinapaswa kuuzwa kwa kutumia gunia au mfuko usiozidi kilo 50, Caroline alisema serikali ya Kaunti ya Meru inaendelea kuhamasisha wakulima manufaa ya kanuni hizo. 

“Tunataka kuanza usajili wa wakulima wa viazi, ili tukianza kutekeleza sheria hizo itakuwa rahisi,” akaelezea. Uholanzi imekuwa ikishirikiana na Kenya kwa karibu kuboresha uzalishaji wa viazi nchini.

  • Tags

You can share this post!

Fimbo ya maaskofu yawaumiza

Chini ya asilimia 10 ya mazao ya shambani yanayouzwa nje ya...