• Nairobi
  • Last Updated March 29th, 2024 3:04 PM
Risasi mazishini ililenga kuniangamiza – Wetang’ula

Risasi mazishini ililenga kuniangamiza – Wetang’ula

Na WAANDISHI WETU

POLISI wanachunguza madai kwamba Seneta wa Bungoma, Bw Moses Wetang’ula ndiye aliyekuwa akilengwa na risasi zilizofyatuliwa katika mazishi aliyohudhuria Jumatatu.

Bw Wetang’ula alikuwa miongoni mwa viongozi katika mazishi ya dereva wa Mbunge wa Likuyani, Bw Enock Kibunguchy, katika Kaunti ya Trans Nzoia.

Kiongozi huyo wa Chama cha Ford-Kenya na kiongozi mwingine wa eneo hilo aliyejeruhiwa katika fujo hizo walidai risasi zilizofyatuliwa zililenga kumwangamiza.

“Niliona polisi ambaye alimpiga risasi diwani na alikuwa akinyoosha bunduki upande wetu. Ninaamini risasi hiyo ililenga kuniangamiza,” akadai Bw Wetang’ula.

Dereva wa Bw Kibunguchy alipigwa risasi akafariki wiki iliyopita katika mkahawa ulio soko la Soy, Kaunti ya Kakamega alipokuwa na mbunge huyo.

Wapelelezi jana walimwagiza mbunge huyo kuandikisha taarifa kuhusu madai yake kwamba mauaji ya dereva wake hayakutokana na uhalifu wa kawaida bali ilikuwa ni njama ya kisiasa kumwangamiza.

Walimtaka aeleze zaidi kile alichomaanisha alipodai kuwa wapinzani wake wa kisiasa ndio walihusika katika shambulio hilo.

Afisa wa Upelelezi wa Jinai katika kaunti hiyo, Bw John Onyango, alisema wanamtarajia Bw Kibunguchy aende katika makao makuu ya polisi hii leo kuandikisha taarifa.

Baadhi ya madiwani katika kaunti hiyo wakiongozwa na Kiongozi wa Wengi katika Bunge la Kaunti, Bw Joel Otwoma, walimlaumu Bw Kibunguchy kwa kuchochea waombolezaji kumfurusha Waziri wa Huduma za Kijamii, Bw Robert Kundu Mukhanu, punde alipowasili mazishini na kusababisha vurugu.

You can share this post!

DIGIFARM: Ithibati tosha teknolojia ndiyo suluhu ya baa la...

Fedheha Ushuru FC kukosa jezi za kuchezea

adminleo