• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 6:50 PM
UDAKU: Alli aweka tangazo kwenye apu kusaka sogora wa mahabubu

UDAKU: Alli aweka tangazo kwenye apu kusaka sogora wa mahabubu

Na CHRIS ADUNGO

KIUNGO matata wa Tottenham Hotspur, Dele Alli, 24, sasa amejisajili rasmi na programu ya mitandaoni, Raya, ili kutafuta mpenzi.

Mwanasoka huyo raia wa Uingereza anafikia uamuzi wa kujiunga na ‘App’ hiyo inayohusishwa na mabwanyenye wiki kadhaa baada ya kutemwa na mwanamitindo Ruby Mae.

Chini ya picha yake akiwa amevalia suti ya rangi ya samawati iliyokolea, Alli alielezea kwamba anamsaka kidosho wa kisasa mwenye mapenzi ya dhati. Aidha, alifafanua kwamba atavutiwa zaidi na demu aliye na sura ya haiba na kifua kilichojaa.

Alli anakuwa supastaa wa hivi karibuni kujiunga na ‘App’ ya Raya baada ya Cara Delev­ingne, Paul Mescal, Lewis Capaldi, Adele na Ben Affleck.

Nyota huyo anayehemewa pakubwa na Paris Saint-Germain (PSG) ya Ufaransa, amesalia kapera baada ya kuponzwa na michezo ya video pamoja na vibonzo vya mitandaoni.

Alitemwa na Ruby, 24, kwa madai kwamba alikuwa akitumia muda wake mwingi kushiriki michezo ya mitandaoni na kumwacha mchumba wake akichapwa na kijibaridi cha upweke usiku kucha. Wawili hao wamekuwa katika mizozo ya mara kwa mara tangu walipoanza kula bata.

Ruby alifunganya virago vyake na kuondoka kwenye kasri la Sh300 milioni linalomilikiwa na Alli jijini London, Uingereza mwanzoni mwa Machi 2021.

Kipusa huyo alidai kuwa alichoshwa na mienendo ya Alli ambaye alikuwa na mazoea ya kuzamia sana michezo ya video aina ya Fortnite.

Kwa mujibu wa gazeti la The Sun, uhusiano kati ya Alli na Ruby ulianza kusambaratika wakati wa maadhimisho ya Siku ya Wapendanao (Valentine’s Day) mwaka huu na wawili hao walipokatiza mawasiliano yao kupitia mitandao ya kijamii mara moja.

Ruby ambaye amewahi kuwa balozi wa mauzo wa bidhaa za Dolce & Gabbana pamoja na Chanel, alianza kutoka kimapenzi na Alli mnamo 2016 na wakatengana kwa mara ya kwanza mnamo 2018 kabla ya kurudiana.

Akihojiwa na gazeti la The Mirror wakati huo, Ruby alisema kiini cha kutengana kwao wakati huo ni jicho kali la nje la Alli ambaye alianza kumtambalia kimapenzi mwigizaji maarufu Megan Barton-Hanson anayemzidi umri kwa mwaka mmoja.

Alli alianza kutoka kimapenzi na Megan mwezi mmoja baada ya kichuna huyo mwenye umri wa miaka 25 kutemana na mwigizaji mwenzake wa filamu za Love Island, Wes Nelson, 22.

Ruby alieleza pia kufadhaishwa pakubwa na mabadiliko ya tabia za Alli ambaye amekuwa mwepesi wa kushiriki ulevi na kula uroda na makahaba wa kila sampuli katika sehemu za burudani.

Uhusiano kati ya Alli na Ruby ulifichuka kwa mara ya kwanza mnamo 2016 baada ya kichuna huyo kuonekana peupe akimpiga busu mwanasoka huyo katika jaribio la kumliwaza baada ya Uingereza kuzamishwa 2-1 na Iceland kwenye fainali za Euro 2016 nchini Ufaransa.

You can share this post!

Watatoboa siasani?

UDAKU: Drinkwater akaukiwa baada ya kutemwa