• Nairobi
  • Last Updated April 25th, 2024 3:34 PM
Droo ya KPL Top 8 sasa ni hadi Machi

Droo ya KPL Top 8 sasa ni hadi Machi

Kocha Robert Matano baada ya kushinda kombe la KPL Top 8 mnamo 2013. Picha/ Maktaba

Na CHRIS ADUNGO

DROO ya kipute cha kuwania ubingwa wa taji la KPL Top8 mwaka imeahirishwa hadi mwezi Machi 2018. Kivumbi hicho kilikuwa kimepangiwa kuanza rasmi Februari baada ya waratibu kuthibitisha kurejea kwa mapambano hayo yanayokutanisha vikosi vilivyokamilisha kampeni za Ligi Kuu katika msimu uliopita ndani ya mduara wa nane-bora.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa jana na KPL, michuano ya Top 8 kwa sasa imesogezwa kwa kipindi cha mwezi mmoja ili kuwapa waratibu wakati maridhawa wa kukamilisha maandalizi muhimu.

Muhoroni Youth ambao waliteremshwa daraja kushiriki kampeni za Ligi ya Daraja la Kwanza msimu huu baada ya kukokota nanga mkiani mwa jedwali la KPL mwaka jana ndio mabingwa washikilizi wa taji la Top 8. Kikosi hicho kiliwabamiza Gor Mahia 1-0 kwenye fainali ya KPL Top 8 mnamo 2016.

Mnamo 2017, KPL ilifutilia mbali kivumbi hicho cha Top 8 katika kalenda yao ya mwaka huo. Kwa mujibu wa Jack Oguda ambaye ni Afisa Mkuu Mtendaji wa KPL, kiini cha kutosakatwa kwa kivumbi hicho msimu huo ni hatua ya kujiondoa kwa waliokuwa wadhamini wakuu wa michuano hiyo, SuperSport .

 

Uhaba wa fedha

Kufutiliwa mbali kwa kipute hicho kwa pamoja na mashindano ya KPL kwa chipukizi wasiozidi umri wa miaka 20 na 16 (KPL U-20 na U-16) kutokana na uchechefu wa fedha kulikuwa pigo kubwa kwa maendeleo ya soka ya humu nchini.

Licha ya kusisitizia kwamba vinara wa klabu za zitakazoshiriki kipute cha Top 8 msimu huu wameshauriwa kupunguza gharama za matumizi kwa minajili ya kivumbi hicho, waratibu wa mapambano hayo wameshikilia kuwa wamepania kutafuta wadhamini wa ziada watakaofadhili nyingi za shughuli zao.

Kipute cha KPL Top8 mwaka huu kitawashirikisha Gor Mahia, Sofapaka, Kariobangi Sharks na Posta Rangers, Kakamega Homeboyz, Tusker, Ulinzi Stars na AFC Leopards.

 

You can share this post!

Runinga ya KTN kupeperusha gozi la Gor dhidi ya Zoo

Maandalizi ya Stars U-20 yakosa kung’oa nanga tena

adminleo