• Nairobi
  • Last Updated April 20th, 2024 3:03 PM
MAWAIDHA YA VALENTINE DEI: Uchu wa ngono  si mapenzi kamwe!

MAWAIDHA YA VALENTINE DEI: Uchu wa ngono si mapenzi kamwe!

Na BENSON MATHEKA

Kwa Muhtasari:

  • Kulingana na Kate, Rich alikuwa gwiji chumbani. Lakini tangu akutane na Deno mambo yamebadilika
  • Sio watu wengi wanaoweza kutofautisha mapenzi ya dhati, tamaa na uchu wa ngono japo wanadai kuwa katika mapenzi
  • Watu wengi hawajipatii muda kuwawezesha kuwa na hakika ikiwa hisia zao kwa wenzao ni za mapenzi ya dhati au uchu wa ngono
  • Mtu akiwa kwenye mapenzi ya dhati mwili hutoa homoni kama vile Oxytocin inayofahamika kuwa homoni ya mapenzi

FEBRUARI 14, 2018 ikiwa Siku ya Wapendanao Kate anafurahi kwamba ametambua maana ya mapenzi ya dhati. Kwa miaka minne kabla ya kukutana na Deno, Kate alikuwa kwenye uhusiano na Rich.

Wakati huo alidhani alikuwa akimpenda Rich sana. Walikuwa wakifanya mapenzi na kulingana naye, Rich alikuwa gwiji chumbani. Hata hivyo, tangu akutane na Deno mambo yamebadilika.

Kate anahisi tofauti sana. Anamfikiria Deno kila wakati na hawezi kumtoa katika mawazo yake. “Nafikiri ninampenda kwa dhati. Napenda kila kitu kumhusu japo hana mapato kama Rich,” asema Kate.

Kulingana na watalaam wa masuala ya mapenzi, sio watu wengi wanaoweza kutofautisha mapenzi ya dhati, tamaa na uchu japo wanadai kuwa katika mapenzi.

 

Ni uroda tu

Wanaonya watu kutoamini kwamba wanaowashehenezea sifa za mapenzi Siku ya Wapendanao wanawapenda kwa dhati wakisema wanachotaka wengi ni kula uroda tu.

“Kuna mambo matatu ambayo huwa vigumu kutofautisha. Kuna mapenzi ya dhati, kumtamani mtu kwa sababu ya kitu fulani unachotaka kutoka kwake na uchu ambao watu hudhani ni mapenzi ya dhati,” asema Darius Mnyala wa Shirika la Big Hearts jijini Nairobi.

Anasema mapenzi ni hisia zenye nguvu kutoka moyo wa mtu. Hisia zinazoteka mtu hadi anashindwa kujielewa. “Sawa na hisia zingine, hisia za mapenzi huwa tofauti kwa watu kwa kutegemea umri na aina ya uhusiano wao na pia mtu binafsi,” asema Bw Mnyala.

Anasema kuna tofauti ya kumpenda mtu na kufanya mapenzi na mtu. “Kupenda mtu ni tofauti na kufanya mapenzi na mtu. Kuwa na mapenzi na mtu ni hisia kali ya ndani kwa ndani ambayo haiwezi kuepukika mwanzo wa uhusiano.

Ukiwa kwenye mapenzi na mtu, unaona uzuri wake kila wakati. Hisia kama hizi huwa kali na nzito kiasi cha kusababisha maumivu hasa ikiwa mtu unayempenda hana hisia kama zako,” asema Bw Mnyala.

 

Mapenzi ya dhati 

Joyce Wariara, mshauri wa kituo cha Love Paradise anasema hisia za mapenzi ya dhati huwa zinajijenga kwa wakati na kisha kukita mizizi ndani ya mtu na kuanza kuchanua na kunawiri.

“Watu wengi hawajipatii muda kuwawezesha kuwa na hakika ikiwa hisia zao kwa wenzao ni za mapenzi ya dhati au uchu wa ngono. Wanapeana mili yao kwa kila mtu anayewashawishi kufanya mapenzi wakidhani wako katika mapenzi ya dhati. Uchu wa kufanya mapenzi si mapenzi ya dhati kamwe. Haya ni mambo tofauti,” aeleza Bi Wariara.

Kulingana na wataalamu, mapenzi ya dhati hujijenga kwa hatua japo si lazima hatua hizo ziwe kwa mpangilio maalumu.

“Kwa kawaida, mapenzi huanza kwa kuhisi mvuto, kisha ndoto na kulemewa na hisia za mapenzi kuhusu mtu fulani na hatimaye kushindwa kumtoa mtu huyo katika moyo wako. Hali kama hii inaweza kuwaunganisha watu wawili katika maisha yao yote,” asema Bw Mnyala.

 

Huoni ubaya

Ukiwa katika mapenzi ya dhati huwa unamfikiria mtu wako siku yote na kufurahia kila kitu anachofanya. Aidha unahisi kuwa na furaha na hauoni ubaya wa mtu wako.

Unamvumilia na kumsaidia katika kila hali tofauti na uchu ambao ni wa muda tu. “Ukitaka kujua umetekwa kimapenzi, huwa unapata hisia za ajabu ukimuona, hisia ambazo huwezi kuzieleza. Unatabasamu kila wakati ukimuona au kusikia sauti yake. Unataka kufanya kila kitu ili kumfurahisha,” asema Bi Wariara.

Hata hivyo, mtaalamu huyu asema kwa baadhi ya watu, ni vigumu kutofautisha mapenzi ya dhati na tamaa ya kimwili. “Unaweza kuongozwa na tamaa na hata kushiriki tendo la ndoa na kulifurahia lakini uwe haumpendi kamwe,” aeleza Bi Wariara.

 

Homoni ya Oxytocin

Wataalamu wanasema mtu akiwa kwenye mapenzi ya dhati mwili hutoa homoni kama vile Oxytocin inayofahamika kama homoni ya mapenzi.

“Ni homoni hii inayofanya mtu kuhisi tofauti akimuona, kumsikia, kumkosa au kuwa na mtu anayependa kwa dhati,” aeleza Bw Mnyala.

Anasema kuna tofauti ya kupenda mtu na kufanya mapenzi. “ Kushiriki tendo la ndoa kunafahamika kama kufanya mapenzi kwa sababu ni sehemu ya uhusiano wa kimapenzi.

Lakini mapenzi na tendo la ndoa ni tofauti sana, unaweza kuwa na moja bila nyingine. Watu wengi hushiriki tendo la ndoa na mtu wanayempenda lakini pia unaweza kula uroda kwa sababu ya uchu.

Hata hivyo wanaofurahia tendo la ndoa kwa dhati ni wanaoburudishana na mtu wanayempenda,” asema Bw Mnyala.

 

You can share this post!

FATAKI: Si lazima kuzaa au kuolewa ndipo ukamilike kama...

Maadhimisho ya Siku ya Valentino yanoga

adminleo