• Nairobi
  • Last Updated April 20th, 2024 7:55 AM
Filamu ya kimataifa ‘Black Panther’ yazinduliwa jijini Kisumu

Filamu ya kimataifa ‘Black Panther’ yazinduliwa jijini Kisumu

Mwigizaji maarufu kutoka humu nchini Lupita Nyong’o (kushoto) akiigiza katika filamu mpya ya kimataifa ‘Black Panther’. Picha/ Hisani

NA CECIL ODONGO

FILAMU ya aina yake ya muigizaji maarufu nchini Lupita Nyong’o ‘Black Panther’ ilizinduliwa Jumanne rasmi kwa mara ya kwanza humu nchini na Afrika nzima kwenye hafla ya haiba kubwa iliyoandaliwa jijini Kisumu.

Lupita mwenye umri wa miaka 34, anatazamwa kama muigizaji bora kutoka bara la Afrika kwenye jukwaa la sinema za Hollywood.

Kuandaliwa kwa onyesho hilo hapa nchini ni njia moja ya kumpa heshima na kumtunuku kwa juhudi zake zilizomfikisha kwenye anga za juu za uigizaji.

Japo mshindi huyo wa tuzo za Oscar hakuhudhuria sherehe hiyo, viongozi wa kaunti ya Kisumu wakiongozwa na Naibu Gavana wa Kisumu Mathews Owili, waziri wa Michezo na Utamaduni kwenye kaunti Bi Achi Ojany Alai miongoni mwa wageni wengine mashuhuri kutoka ndani na nje ya nchi walikUwepo kushuhudia tukio hilo la kihistoria.

Ratiba ya Lupita iliwa na shughuli nyingi kwa hivyo hangeweza kupata muda wa kufika nchini.

 

Ujasusi

Kwenye sinema ‘Black Panther’ Lupita huigiza kama mhusika Nakia ambaye ni jasusi kwenye ufalme unaoitwa Wakanda. Yeye ni moja wa wa wenye usemi mkubwa kwenye familia ya Wakanda.

Ilikuwa ni fahari kubwa kwa mji wa Kisumu kuteuliwa kuandaa uzinduzi huo wa kwanza Afrika japo kuna miji kadhaa ya hadhi barani. Kaunti ya Kisumu ndiko anakotoka mwigizaji Lupita na babake Prof Peter Anyang’  Nyong’o ambaye ndiye gavana.

Hoteli nyingi za mji huo zilizaa wageni huku tiketi za ndege kuelekea mji huo kutoka kwingineko zikichukuliwa zote na wasafiri walioenda kushuhudia uzinduzi huo.

Vyombo vya habari vya kimataifa na vya ndani ya nchi pia havikusazwa kwa kuwa vyote vilikuwepo kunasa matukio yote.

Kutakuwa na utazamaji wa sinema hiyo Jumatano Siku ya Wapendanao kule Anga Sky Cinema, Nairobi na shoo ya kwanza kwa umma itafanyika Alhamisi Anga IMAX.

Uzinduzi huo aidha umetuliza joto la kisiasa katikakaunti hiyo anakotoka kinara wa NASA Raila Odinga aliyeapishwa kuwa ‘rais wa wananchi.’

Wakazi wa kaunti hiyo walionekana kufurahia kumuona mmoja wao akiigiza katika filamu ya Hollywood, hali iliyoondoa fikra za kisiasa katika Siku ya Valentino.

You can share this post!

FUNGUKA: ‘Amenigeuza ngoma ila nampenda kupindukia’

Marwa kusimamia Kombe la Dunia Urusi

adminleo