• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 8:27 PM
Chanzo cha uskwota Pwani ni unyakuzi wa ardhi – Ripoti

Chanzo cha uskwota Pwani ni unyakuzi wa ardhi – Ripoti

Mwenyekiti wa Tume ya Kitaifa ya Ardhi Dkt Muhammad Swazuri. Picha/ Maktaba

Na KAZUNGU SAMUEL

KISA cha majuzi katika Kaunti ya Kwale ambapo watu kutoka Nairobi walivamia ranchi moja na kudai kuimiliki, ni mojawapo ya visa vinavyoonyesha kusambaa kwa shida za mashamba katika ukanda wa Pwani.

Kulingana na mshirikishi wa masuala ya ardhi katika ukanda wa Pwani, Bw Nagib Shamsan, tatizo la uskwota na mashamba Pwani linaendelea kwa kuwa hakuna serikali ambayo iko tayari kulishughulikia.

“Mwaka wa 2009 kulikuwa na ripoti ya Jopo la Njonjo ambalo ilibuniwa kuchunguza kwa kina shida za mashamba katika ukanda wa Pwani.

Nilihusika pakubwa katika kutayarisha ripoti hiyo na ilikuwa na mapendekezo makubwa ambayo yangetatua shida za mashamba Pwani,” akasema Bw Shamsan kwenye mahojiano na Taifa Leo jijini Mombasa.

Afisa huyo alisema kuwa ripoti hiyo ililenga sana eneo la Maili Kumi katika ukanda wa Pwani ambako visa vya watu kuvamia mashamba na kudai ni ya mababu zao vimezagaa.

Katika ripoti hiyo, iligundulika kuwa ni familia chache ambazo zinamiliki ardhi katika ukanda wote wa Pwani huku wakazi wengi wakiwa maskwota. Visa hivyo vingi vinapatikana katika kaunti za Kilifi, Mombasa na Kwale.

“Katika ripoti hiyo tuligundua kwamba kuna familia 128,900 ambazo ni maskwota katika eneo la Pwani. Wenye mashamba wasiokuwepo wanamiliki ekari 77,753 za mshamba katika eneo la Pwani.

Ni mashamba haya ambayo yamekuwa kiini cha mizozo kati ya wakazi na maajenti wa wamiliki hao. Wengi wa wamiliki wanaishi katika mataifa ya Kiarabu,” akasema Bw Shamsan kwenye mahojiano yetu.

 

Lawama

Hata hivyo, alilaumu serikali kwa kushindwa kumaliza shida ya mashamba katika eneo la Pwani licha ya kuwa na uwezo wa kuweza kutimiza hilo.

Naye afisa mkuu wa shirika la Kenya Land Alliance,  Bw Odenda Lumumba alisema kwenye mahojiano yetu kwamba serikali imeamua kupuulizia mbali suala la ardhi katika eneo la Pwani.

Alisema serikali inafahamu  fika jinsi inavyoweza kumaliza shida hiyo lakini kutokana na ulegevu, imeamua suala hilo libakie kama donda ndugu kwa Wakenya.

“Hivi majuzi, Tume ya Ardhi nchini (NLC) kupitia kwa mwenyekiti wake Prof Muhhamad Swazuri ilitangaza kwamba itaanza kuchukua ardhi za mabwenyenye na kuwagawanyia wananchi.

Lakini lazima tufahamu kuwa Prof  Swazuri na wengine waliowahi kushughulikia suala la ardhi walisema na bado hakuna kitu ambacho wametekeleza.

Serikali haina nia ya kumaliza shida za mashamba katika Pwani,” akasema Bw Lumumba.

 

You can share this post!

Jeshi latoa ahadi ya kusajili wanawake zaidi siku zijazo

Tobiko aanza kazi kwa kuonya wafanyabiashara haramu wakatao...

adminleo