• Nairobi
  • Last Updated April 19th, 2024 1:14 PM
Onyo Nzoia Sugar yaweza kushushwa daraja

Onyo Nzoia Sugar yaweza kushushwa daraja

Na CECIL ODONGO

HUKU ligi kuu hapa nchini ikiingia mechi za raundi ya nne wikendi hii kikosi cha soka cha timu ya Nzoia Sugar bado kinasuasua baada ya kupoteza mechi zao zote.

Vijana hao wa Kocha Bernard Mwalala wamepoteza mechi zote tatu licha ya kuhimili mawimbi makali msimu uliopita na kumaliza wa tisa kwenye msimamo wa jedwali la KPL.

Walichapwa 1-0 na klabu ya Kariobangi Sharks mechi ya kwanza, 2-1 na Mathare United kisha 1-0 na Nakumatt FC wikendi iliyopita.

Timu ya Nzoia pamoja na wenzao Homeboys ndizo timu za pekee kutoka uliokuwa mkoa wa Magharibi wanaoshiriki ligi kuu ya KPL. Klabu ya Western Stima iliyokuwa ikishiriki ligi hiyo ilishushwa daraja mwisho wa msimu jana walipomaliza kwenye nafasi ya 17.

Kulingana na Kocha Benard Mwalala ubutu wa washambulizi wake mbele ya lango la wapinzani ndio umewafanya kutopata matokeo mazuri.

Mastraika wake wamefanikiwa kuwafungia mabao manne pekee nao wapinzani wao kwenye mechi zote tatu wakiwafunga mabao tisa.

Msimu uliopita baada ya kutesa mara tatu ligi ikianza Nzoia sugar walikuwa na alama nne.Mwanzo huo wa wastani kwenye ligi hiyo uliwapa motisha na wakaepuka kushushwa daraja.

Kwenye dirisha ndogo ya usajili timu hiyo iliamua kudumisha wengi wa wachezaji wake lakini wakawasajli wachezaji wanane miongoni mwao difenda Edwin Wafula kutoka klabu ya western stima, chipukizi Harrison Osotsi kutoka shule ya upili ya Chavakali na Michael Osundwa kutoka Nakuru All stars.

Nzoia wanakabiliwa na kibarua kigumu huku mechi zao mbili zijazo zikiwashuhudia wakitesa dhidi ya klabu ya Tusker ugenini kisha wacheze na majirani wao Kakamega Homeboyz nyumbani.

Timu hiyo inacheza msimu wake wa pili ligini baada ya kupandishwa ngazi mwaka 2016 kushiriki ligi kuu. Mwaka huo walimaliza wa kwanza kwenye super league mbele ya Kariobangi Sharks na Nakumatt FC.

You can share this post!

Watu 10 wanaswa kwenye msako dhidi ya karatasi za plastiki

Atwoli anagawanya jamii ya Abaluhya, aonya Wetang’ula

adminleo