• Nairobi
  • Last Updated April 24th, 2024 10:40 AM
Gharama ya umeme kupanda zaidi kusiponyesha

Gharama ya umeme kupanda zaidi kusiponyesha

Kifaa cha kidijitali cha kuhesabu matumizi ya umeme. Picha/ Maktaba

Na BERNARDINE MUTANU

HALI ya maisha itakuwa ngumu zaidi siku chache zijazo ikiwa mvua haitanyesha, kutokana na ongezeko la gharama ya umeme.

Hii ni kutokana na kuwa maji katika bwawa la Masinga, ambalo ni kubwa zaidi katika uzalishaji wa umeme nchini kwa njia ya maji yamepungua kwa kiwango kikubwa.

Huenda serikali ikalazimika kutumia dizeli kuzalisha umeme, bidhaa iliyo ghali (mara sita zaidi ya stima inayotokana na maji), katika kuzalisha stima ikilinganishwa na maji.

Pia stima kutokana na mvuke ni ghali sana (mara tatu kuliko inayotokana na maji)na huenda gharama ya uzalishaji wa umeme ikahimiliwa na wananchi.

Bwawa la Masinga, na viwanda vingine vya uzalishaji wa stima kwa njia ya maji, limeathiriwa na ukame mkubwa unaoshuhudiwa nchini.

Bwawa la Sondu-Miriu kwa mfano linazalisha umeme nusu ya kiwango chake, kwa sababu ya upungufu mkubwa wa maji.

Kiwango cha maji kikishuka zaidi ya ilivyo kwa sasa katika Bwawa la Masinga, huenda serikali ikalazimika kufunga kiwanda hicho cha kuzalisha umeme, alisema Waziri wa Kawi Bw Charles Keter.

You can share this post!

IEBC yasema inahitaji Sh8 bilioni kutathmini upya mipaka

KenGen kuzalisha megawati 160 kutokana na mvuke

adminleo