• Nairobi
  • Last Updated April 19th, 2024 8:55 PM
Miguna Miguna alikuwa hatari kwa usalama wa nchi, mahakama yaambiwa

Miguna Miguna alikuwa hatari kwa usalama wa nchi, mahakama yaambiwa

Mawakili James Orengo (kulia) , Dkt John Khaminwa na Nelson Havi wanaomwakilisha Dkt Miguna Miguna na wakili wa Serikali Emmanuel Mbittah. Picha/ Richard Munguti

Na RICHARD MUNGUTI

KUTIMULIWA kwa mwanaharakati Dkt Miguna Miguna humu nchini kumeendelea kuibua masuala mbalimbali huku Serikali ikiambia Mahakama Kuu kwamba alikuwa tisho kwa usalama wa nchi.

“Kabla ya uamuzi wa kumfurusha Dkt Miguna kutoka humu nchini, Mkurugenzi wa Idara ya Uhamiaji Bw Gordon Kihalangwa alikuwa amepashwa habari na maafisa wa upelelezi kwamba alikuwa tisho kwa usalama wa kitaifa,” Jaji Enock Mwita aliambiwa na Wakili wa Serikali Emmanuel Mbittah.

Na wakati huo huo Jaji Mwita alifahamishwa mwaka wa 2003 , Dkt Miguna alipata uraia wa Canada na kurudishwa kwake kwao na hakuna makosa yoyote kutokana na ufichuzi kwamba alikuwa anajihusisha na vitendo ambavyo ni hatari kwa usalama wa kitaifa.

Bw Mbittah alimweleza Jaji Mwita kufurushwa kwa Dkt Miguna ni kwa manufaa ya kila mwananchi.

“Bw Kihalangwa alipokea habari kutoka kwa maafisa wa uchunguzi wa jinai kwamba Dkt Miguna alikuwa anajihusisha na visa vilivyo tisho kwa usalama wa kitaifa na ilifaa arudishwe nchini Canada,” Bw Mbittah alisema.

Wakili huyo wa Serikali aliambia mahakama taarifa hizo za wapelelezi zilizojulishwa Bw Kihalangwa, zilielezewa Waziri wa Usalama Dkt Fred Matiang’i ambaye mara moja Dkt Miguna alimtangaza kuwa “mtu asiyetakikana humu nchini.”

Bw Mbittah alisema hakuna sheria yoyote ambayo serikali ilivunja ama kukaidi haki za Dkt Miguna katika kufutilia mbali cheti cha kusafiria cha Dkt Miguna na kumtangaza mtu asiyetakikana.

“Uamuzi wa kumfurusha Dkt Miguna uliochukuliwa na Bw Kihalangwa na Dkt Matiang’i haupasi kukosolewa kwa vile ulikuwa kwa mujibu wa sheria,” Jaji Mwita alifahamishwa.

Mahakama itatoa uamuzi Feburuari 23, 2018.

You can share this post!

Bei ghali ya mafuta kupandisha gharama ya maisha

BI TAIFA FEBRUARI 20, 2018

adminleo