• Nairobi
  • Last Updated March 29th, 2024 11:38 AM
JAMVI: Dhamira fiche ya Uhuru kuzuia wabunge wa Jubilee kuhojiwa yaanikwa

JAMVI: Dhamira fiche ya Uhuru kuzuia wabunge wa Jubilee kuhojiwa yaanikwa

Kumteua Bw Raphael Tuju kama waziri asiyeshikilia nafasi yoyote ni juhudi za kuhakikisha kwamba maslahi ya Chama cha Jubilee (JP) yanashughulikiwa serikalini, na katika wizara zote. Picha/ Maktaba

Na WANDERI KAMAU

Kifupi:

  • Imefichuka kuwa Jubilee ina mipango madhubuti inayoendeshwa kichinichini kuhakikisha kwamba imedhibiti  habari 
  • Imebainika JP pia inabuni mikakati ya kutoa mafunzo maalum kwa maafisa watakaosimamia chama hicho kutoka ngazi za mashinani hadi za kitaifa
  • Huenda ikawa vigumu kwa Kenya kuwa na chama kimoja ama viwili vya kisiasa, ikizingatiwa kwamba mazingira ya kisiasa nchini ni telezi sana
  • Chama hicho kitageuzwa kuwa chenye asasi thabiti ambazo zitahakikisha kimebaki imara, hata wakati UhuRuto watakapoondoka uongozini

 

HATUA ya Rais Uhuru Kenyatta kuwazuia wabunge wa Jubilee kushiriki katika mahojiano yoyote na vyombo vya habari imeibua mkakati wa serikali kuirejesha Kenya katika enzi ya chama kimoja.

Aidha, imefichuka kuwa mkakati huo ni sehemu ya mipango madhubuti inayoendeshwa kichinichini na uongozi wa Jubilee kuhakikisha kwamba imedhibiti jinsi habari muhimu kuhusu maendeleo ya chama hicho yanavyowafikia wananchi.

Mbali na hayo, kuteuliwa kwa Bw Raphael Tuju kama waziri asiyeshikilia nafasi yoyote ni juhudi za kuhakikisha kwamba maslahi ya Chama cha Jubilee (JP) yanashughulikiwa serikalini, na katika wizara zote.

Imebainika kwamba kuwa hiyo ndiyo sababu kuu ambapo Bw Tuju, ambaye pia ni Katibu Mkuu wa JP, hakupigwa msasa na Bunge, kwani wajibu wake ni ‘mkubwa’.

“Wajibu wa Bw Tuju ni kuhakikisha kuwa utendakazi wa kila wizara unawiana na malengo ya Jubilee, hasa manifesto yake. Ni hali ya kawaida, katika nchi zenye vyama thabiti vya kisiasa kama Afrika Kusini, Uchina, Tanzania, Uganda kati ya nchi nyingine,” zikaeleza.

Duru zimeeleza kwamba ili kuhakikisha kuwa hakuna pengo lolote katika uongozi wa chama, Rais Kenyatta ataendelea kuwa kiongozi rasmi wa JP, hata atakapong’atuka uongozini kama rais mwaka wa 2022.

 

Kugeuza Jubilee kuwa KANU

Na ingawa, hilo lingali kubainika kwa wengi, wachanganuzi wanasema kuwa huo ni mpango wa wazi wa kukikuza chama hicho kufikia kiwango cha chama cha Kanu, ambacho kiliitawala nchi kwa karibu miongo mitano.

“Nadhani ni wazi kwamba Jubilee inairejesha Kenya katika enzi ya utawala wa chama kimoja cha kisiasa,” asema Gabriel Otachi, ambaye ni mchanganuzi wa kisiasa.

Imebainika kwamba JP pia inabuni mikakati ya kuweka mchakato wa kutoa mafunzo maalum kwa maafisa watakaosimamia chama hicho kutoka ngazi za mashinani hadi za kitaifa.

Kulingana na mwongozo ulioonwa na Jamvi la Siasa, lengo kuu ni kukiwianisha na vyama Chama cha Kikomunisti cha Uchina (CP), African National Congress (ANC) cha Afrika Kusini, Chama cha Mapinduzi (CCM) nchini Tanzania kati ya vingine vyenye nguvu.

“Lengo la JP ni kubuni utaratibu thabiti wa usimamizi wa chama, ambao utahakikisha kuwa uongozi wake hautegemei uwepo wa mtu binafsi, basi asasi zitakazokuwepo,” unaeleza mwongozo huo.

 

Ni vigumu

Hata hivyo, wachanganuzi wanatilia shaka mpango huo, wakisema kuwa huenda ikawa vigumu kwa Kenya kuwa na chama kimoja ama viwili vya kisiasa, ikizingatiwa kwamba mazingira ya kisiasa nchini ni telezi sana, ikilinganishwa na mataifa mengine.

“Kenya ni nchi iliyostawi sana kidemokrasia. Hivyo, jaribio lolote la kuirejesha katika chama kimoja huenda lisifaulu, kwani watu wataliasi kwa kutumia vipengele vilivyo katika Katiba kudai haki zao,” asema Bw Kipkorir Mutai, ambaye ni mhadhiri wa Sayansi ya Siasa katika Chuo Kikuu cha Egerton.

Hata hivyo, baadhi ya wadadisi wanasema kwamba hawajashtushwa na mpango huo, kwani ilidhihirika tangu awali kwamba mpango wa mabw Uhuru na Naibu Raid William Ruto walikuwa na mipango mikubwa kuigeuza Jubilee kuwa chama chenye nguvu.

“Ilidhihirika awali kwamba mpango wao ulikuwa kubuni chama chenye nguvu, hasa baada ya Jubilee ‘kumeza’ vyama tanzu kama vile TNA, URP na vinginevyo. Hii ilikuwa hatua ya kwanza kwamba lengo lao lilikuwa kubwa zaidi,” asema Bw Mutai.

Vile vile, wachanganuzi pia wanataja ukaribu uliopo kati ya uongozi wa Jubilee na CP kutoka Uchina, kama ishara ya wazi kwamba haiangalii nyuma.

Mwezi uliopita, ujumbe kutoka CP uliwasili nchini, ambapo ulitoa mafunzo kwa maafisa kadhaa wa Jubilee. Ilibainika kwamba maafisa hao watatumiwa na chama kuendesha ajenda zake katika kutoka ngazi ya kitaifa hadi mashinani.

Ilibainika kwamba jukumu kuu la maafisa hao litakuwa kuwafikia wananchi katika viwango vyote ili kuwafahamisha kuhusu ajenda kuu za chama, hasa manifesto yake.

 

Kuimarisha chama

Katika mojawapo ya mahojiano na kituo kimoja cha televisheni majuzi, mwenyekiti wa JP Bw David Murathe alieleza kuwa chama hicho kitageuzwa kuwa chenye misingi na asasi thabiti ambazo zitahakikisha kwamba kimebaki imara, hata wakati Rais Kenyatta na Bw Ruto watakapoondoka uongozini.

“Hatuna nia mbaya, ila lengo letu kuu ni kuimarisha mfumo wa siasa za nchi, ili kuondoa utegemezi wa watu binafsi, ila uwepo wa vyama ambavyo vitaendeleza malengo yake, hata viongozi hao watakapoondoka,” akasema Bw Murathe.

Mwezi uliopita, Rais Kenyatta alihudhuria maadhimisho ya miaka 106 tangu kuanzishwa kwa ANC, Afrika Kusini, hatua iliyoonekana kuimarisha ushirikiano kati ya vyama hivyi viwili.

Licha ya hayo, wakosoaji wa mpango huo wanautaja kama njama ya kurejesha utawala wa kidikteta nchini. Wanazikosoa mbinu hizo, hasa kuwazuia wabunge kutoa hisia zao kuhusu hali ya nchi, kama ishara ya wazi ya ukiukaji wa haki za kujieleza.

“Sitashangaa ikiwa nitaona maasi kutoka ukanda wa Mlima Kenya (anakotoka Rais Kenyatta) ama Bonde la Ufa (anakotoka Bw Ruto) kwani huu ni udikteta wa wazi,” akasema mwanaharakati wa kisiasa Raymond Mutembei.

 

You can share this post!

JAMVI: Dhana Raila atawania urais 2022 yazua hofu ya...

JAMVI: Sababu ya Uhuruto kufurahia ukaidi wa Raila kwa...

adminleo