• Nairobi
  • Last Updated April 24th, 2024 8:12 PM
Shoo ya #WifeMaterial yamtia Eric Omondi matatani

Shoo ya #WifeMaterial yamtia Eric Omondi matatani

Na SAMMY WAWERU

Mcheshi maarufu Eric Omondi amejipata matatani kutokana na shoo yake ya #WifeMaterial. Shoo hiyo tata imekuwa ikimhusisha na wanawake kadhaa, ambapo amekuwa akionekana akiwabusu na kuwakumbatia hadharani, kupitia video na picha anazopakia kwenye kurasa zake za mitandao ya kijamii.

#WifeMaterial, kulingana na machapisho ya Erico, imekuwa droo ya mashindano ya “mwanamke bora kwenye ndoa”, na ambayo kilele chake kilikuwa mnamo Jumatano, Desemba 23, 2020 alipotangaza mshindi.

“Na mshindi ni…” mvunja mbavu huyo tajika akachapisha katika kurasa zake za mitandao.

Jumatano hiyohiyo, Omondi alipakia video anayoonekana akiwa na ng’ombe jijini. “Vile tunapeleka mahari kwa kina mshindi wa #WifeMaterial,” yanasema maelezo ya video hiyo.

Shoo hiyo imeonekana kughadhabisha Afisa Mkuu Mtendaji wa Bodi ya Kukagua Filamu Nchini (KFCB), Dkt Ezekiel Mutua, akiitaja kama “iliyooza, potovu na inayochangia utovu wa maadili kwa wasichana”.

“Kuna Corona, lakini huyu ‘mjinga’ amekuwa akibusu wasichana kadhaa, akinasa video kwa madai anaigiza. Msosholaiti mwingine naye, aliyepotoka anarekodi video zaidi akifunza wasichana wadogo jinsi ya kufanya mapenzi na Omondi kupitia programu ya kishetani inayojulikana kama ‘Mombasa Raha’…” ameeleza Dkt Mutua.

Akionekana kukerwa na tabia za Erico, Afisa huyo mwenye msimamo mkali kuhusu masuala ya filamu na uigizaji nchini, anataja studio ya mchekeshaji huyo iliyoko mtaani Lavington, Nairobi, kama ngome ya kudhulumu wasichana kimapenzi na kuwashushia hadhi yao kwa madai ya kuimarisha sekta ya uigizaji.

“Huku mashirika ya kutetea haki za wanawake yakinyamaza na idara ya polisi kutokamata wahusika wa uhalifu huu, ni bayana kama jamii tumepotoka,” Dkt Mutua anasema.

Akiitaka idara ya Uchunguzi wa Jinai (DCI) kukamata wahusika, anasema wakati taifa litapevuka kwa maovu hayo, athari ambazo zitakuwa vigumu kurekebisha zitakuwa zimetendeka.

Si mara ya kwanza Dkt Mutua kutofautiana vikali na Eric Omondi, akimtaka kuwa kielelezo na mfano mwema katika jamii kupitia umaarufu wake kwenye uigizaji.

Mitandaoni, kuna baadhi ya wanaosifia shoo ya Erico na wengine wakimkashifu.

“Erico usiombe yeyote msamaha, tuko kwenye dunia huru, hukulazimisha yeyote kushiriki. Wasichana walijitolea kushiriki mashindano kwa hiari yao…” anaeleza Adrian Akasha.

“Tunataka hatua ichukuliwe mara moja, hatutaki mazungumzo,” #Makori Douglas anapendekeza.

“Erico anaonekana kupambana na msongo wa mawazo baada ya mchumba wake wa Kiitaliano kumuacha,” #Chepngeno Benta anadai.

You can share this post!

Krismasi bila shangwe

Wakazi wa Mombasa wafurahia daraja jipya la kuelea Liwatoni