• Nairobi
  • Last Updated April 20th, 2024 3:03 PM
Sh19 bilioni za mpango wa elimu bila malipo kutolewa kabla ya Januari 4

Sh19 bilioni za mpango wa elimu bila malipo kutolewa kabla ya Januari 4

Na CHARLES WASONGA

WIZARA ya elimu Jumatatu ilitangaza kuwa serikali itatuma Sh19 bilioni katika shule za msingi na za upili za umma chini ya mpango wa elimu bila malipo kabla ya shule kufunguliwa Januari 4, 2021.

Waziri wa Elimu George Magoha alisema mazungumzo yanaendelea kati ya Wizara yake na ile ya Hazina ya Kitaifa kuhakikisha kwamba fedha hizo zinatumwa “haraka iwezekanavyo”.

Profesa Magoha alisema Sh4 vilioni kati ya fedha hizo zitaelekezwa kwa shule za msingi huku Sh15 bilioni zikitumwa kwa shule za upili.

Akiongea katika shule ya upili ya Obola iliyoko eneo bunge la Seme, kaunti ya Kisumu alipokagua mradi wa msambazaji madawati, Profesa Magoha aliwataka walimu wakuu kuhakikisha kuwa fedha hizo zimetumika vizuri. Alionya kuwa wale watakaopunguza fedha hizo watachakuliwa hatua za kinidhamu bila kuhurumiwa.

“Serikali imeweka mikakati hitajika ya kuhakikisha kuwa shule zinafunguliwa ikiwamo kusambazwa kwa fedha za mpango wa elimu bila malipo kwa wakati kabla ya masomo kuanza,” akasema.

Profesa Magoha akaongeza: “Nawaomba wazazi kutowatuma nyumbani wanafunzi kwa kukosa karo, bali washughulikie mchangamoto zinazowakabiliwa wazazi, mmoja baada ya mwingine.”

Waziri alisema janga la Covid-19 limewaathiri waziri kiuchumi na kuwataka walimu wakuu kutowawekea wazazi mahitaji makubwa.

“Lakini nawaomba wazazi kuwakagua wazazi kwa sababu kuna baadhi yao ambao ni waongo na huenda wakazingizia changamoto ya kiuchumi inayoshuhudiwa nchini kukwepa kulipa karo ya watoto ilhali wanayo uwezo wa kifedha,” Profesa Magoha akasema.

Profesa Magoha alisema serikali imewatambua wanafunzi milioni 3 kutoka jamii masikini ambao watapewa barakoa bila malipo.

“Tayari tuko na maski milioni mbili ambazo zitasambaziwa watoto kutoka familia masikini. Isitoshe, tunafanya mazungumzo na kampuni ya kutengeneza ngua ya Rivatex iwasilishe maski milioni moja zilizosalia kabla ya shule kufunguliwa,” akaeleza.

Profesa Magoha alikiri kuwa itakuwa vigumu kwa shule kudumisha kanuni ya kutenganisha wanafunzi na ndipo akawataka wazazi kuhakikisha kuwa watoto wao wanavalia maski nyakati zote kuhusu msambao wa Covid-19 shule zitakapofunguliwa.

Kuhusu mradi wa madawati shuleni, Profesa Magoha alisema kufikia Jumatatu, Desemba 28, 2020, madawati 500,000 yalikuwa yamesambazwa katika shule mbalimbali za umma nchini.

“Maafisa wa serikali wakiwemo wale elimu, wenzao kutoka wizara ya masuala ya ndani na viongozi wa kisiasa watahakikisha kuwa mafundi wa Jua Kali wanaotengeneza madawati hayo wameyawasilisha shuleni kufikia Jumatatu,” akaeleza.

Wakati huo huo, Profesa Magoha ametangaza kuwa watoto ambao wamekuwa wakisoma katika shule za kibinafsi zilizofungwa watahamishwa hadi katika shule za umma.

“Na mikakati imewekwa kuhakikisha kuwa watahiniwa kutoka shule hizo wanafanya mitihani yao ya kitaifa katika vituo vya serikali,” akasema.

You can share this post!

Muthama na Koech wataka walipwe fidia baada ya kukamatwa

NCIC yasema haitawashtaki Sifuna na Jumwa