• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 11:33 AM
NCIC yasema haitawashtaki Sifuna na Jumwa

NCIC yasema haitawashtaki Sifuna na Jumwa

Na CHARLES WASONGA

KATIBU Mkuu wa ODM Edwin Sifuna na Mbunge wa Malindi Aisha Jumwa wamesamehewa kwa kosa la kulumbana kwa kutumia maneno machafu na yanayoweza kuchochea chuki na uhasama wa kijaa wakati wa kampeni za kuelekea uchaguzi mdogo wa eneo bunge la Msambweni.

Tume ya Uwiano na Utangamano wa Kitaifa (NCIC) Jumatatu ilisema kuwa haitawafungulia mashtaka wawili hao. Hii ni baada ya wawili hao kuomba msamaha hadharani kufuatia matamshi hayo.

“Kwetu hatutaendelea na kesi hii zaidi yale tumefanya,” akasema Kamishna wa NCIC Danvas Makori.

Kamishna huyo alisema kwamba kwa kuwa wanasiasa hao wawili waliungama makossa yao na kutoa msahama kwa umma ni ishara kwamba wamesikitikia makossa yao na wako tayari kuridhiana.

“Matamshi yao yangeathiri wafuasi wao. Yangechochea uhasama kati yao. Kwa hivyo, ikiwa wameyaondoa, hiyo ni ishara kwamba wako tayari kufuata mkondo wa maridhiano,” Bw Makori akasema jana, kwenye taarifa.

Kamishna huyo alisema kuwa sheria za NCIC zinawapa mamlaka ya kusitisha mashtaka dhidi ya wachochezi wa chuki ikiwa wataungamana makosa yao hadharani na kuahidi kufuata mkondo wa maridhiano.

“Kipengele cha 51 cha sheria ya NCIC kinaipa tume mamlaka ya kupatanisha pande hasimu.

Bw Sifuna na Bi Jumwa walihojiwa na maafisa wa tume hiyo wiki jana na baadaye wakaomba msamaha hadharani.

“Naomba msamaha kwa matamshi yao yaliyoonekana kusifu dhuluma za kimapenzi zinazofanyiwa wasichana na wanawake. Kama wakili nimejitolea kuwatoa hudumu za kisheria bila malipo kwa saa 50 kwa visa vya dhuluma za kimapenzi haswa vinavyotokea katika eneo bunge la Msambweni. Hii itaonyesha kuwa nimesikitikia matamshi niliyoyatoa,” akasema Jumatatu wiki jana.

Siku moja iliyofuata, Jumanne, Jumwa pia aliomba msamaha na kuapa kwamba hatarudia kosa hilo wakati mwingine.

“Watu hawakujua kile ambacho kilichochea matamshi yangu. Lakini naomba kwa wananchi wote, haswa watoto wa kike.

Mbunge huyo wa Malindi vile vile alisema amemsamehe Bw Sifuna kwa kumshambulia kwa maneno ya aibu na yanayodumisha hadhi yake kama mwanamke na kiongozi.

You can share this post!

Sh19 bilioni za mpango wa elimu bila malipo kutolewa kabla...

Miguna aahidi kuzima ufisadi Nairobi