• Nairobi
  • Last Updated March 19th, 2024 11:34 AM
IEBC yaomba radhi kwa kuita BBI ‘Burning Bridges Initiative’

IEBC yaomba radhi kwa kuita BBI ‘Burning Bridges Initiative’

Na CHARLES WASONGA

TUME Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) Jumatano ililazimika kuomba msamaha baada ya kurejelea mpango wa maridhiano (BBI) kama “Burning Bridges Initiative” badala ya “Building Bridges Initiative”.

Awali, kwenye ujumbe katika akaunti yake ya Twitter, tume hiyo ilitumia maneno hayo kimakosa ilipokuwa ikitangaza kuanza kwa mchakato wa ukaguzi wa sahihi kuunga mkono mageuzi ya Katiba kupitia BBI.

Lakini baada ya Wakenya mitandaoni kulalamika, IEBC ilituma taarifa ikifafanua kuwa ujumbe huo ulitokana na makossa ya tahajia (typographical error) “ambayo haiwakilishi msimamo wa tume hii.”

“Mapema leo (Jumatano), tume hii iliweka ujumbe kuhusu uzinduzi wa zoezi ya ukaguzi wa sahihi za wafuasi wa BBI. Hata hivyo, kulikuwa na hitilafu ya kitahajia kwenye ujumbe huo ambayo hayakukusudiwa. Kosa hili haliwakilisha msimamo wa tume au wafanyakazi wake. IEBC imeomba msamaha kwa wadau wote na umma,” ikasema taarifa hiyo ya kuomba msamaha.

Duru pia zinasema kuwa msimamizi wa akauti ya twitter ya IEBC Jonathan Kiptoo alipiga kalamu kutokana na kosa hilo.

IEBC ilizindua zoezi hilo ambalo litaendeshwa na makarani 400 walioajiriwa kwa ajili ya kibarua hicho baada ya kupokea mafunzo kwa siku moja.

“Makarani hao wamekula kiapo cha usiri ishara kwamba watafanya kazi inavyohitajika kisheria,” mwenyekiti Wafula Chebukati akawaambia wanahabari wakati wa uzinduzi wa shughuli hiyo katika ukumbi wa Bomas of Kenya.

Makarani hao watakiwa wakilipwa ujira wa Sh1,200 kila siku katika zoezi ambapo litagharimu jumla ya Sh480,000 kwa siku na Sh94 milioni hadi litakapokamilika.

You can share this post!

Cavani kuendelea kusakatia Man United hata baada ya msimu...

Wakazi wampiga mwendawazimu wakidai ni mchawi