• Nairobi
  • Last Updated April 19th, 2024 8:55 PM
2020: Waliong’aa na kugusa Wakenya kwa njia ya kipekee

2020: Waliong’aa na kugusa Wakenya kwa njia ya kipekee

Na BENSON MATHEKA

INGAWA mwaka huu umekuwa mgumu kwa Wakenya, kuna waliong’ara katika nyanja mbalimbali na kugusa wengi kwa kuonyesha utu.Baadhi yao walitambuliwa kimataifa na kutuzwa kwa juhudi zao wakiwemo walimu, wafanyakazi, wanafunzi na wanamichezo.

Michael Munene, Landilodi mkarimu

Wakati wamiliki wa nyumba za kukodisha katika maeneo ya mijini walipokuwa wakihangaisha walioshindwa kulipa kodi kufuatia athari za janga la corona, Bw Michael Munene aligusa wengi kwa kuwasamehe wapangaji wa ploti zake katika Kaunti ya Nyandarua kwa miezi minne na hata kuwapa misaada ya chakula.

“Tunafaa kuwa na utu hata kama tunataka pesa. Ulikuwa wakati wa janga nao wapangaji hawakuwa kazini. Niliamua kuwapa afueni kwa sababu ninaelewa masaibu yao. Kama nilivyosema wakati huo, mimi nimewahi kuwa mpangaji na ninaelewa shida za watu,” asema.

Jane Kimiti, mwalimu bora barani Afrika

Mwalimu mkuu wa shule ya wasichana ya Othaya kaunti ya Nyeri alitawazwa mwalimu bora barani Afrika na muungano wa Afrika mwaka huu kwa kubuni mbinu bora za ufundishaji wa wanafunzi.

Bi Kimiti alitambuliwa kwa mbinu za kuhimiza na kuhakikisha wanafunzi wanadumisha nidhamu. Wakati walimu walikuwa wametulia nyumbani baada ya shule kufungwa, Bi Kimiti alianzisha mfumo wa kuhakikisha wanafunzi walikuwa wakiendelea na masomo.

“Tulishirikiana na machifu wa maeneo husika kuendeleza elimu ya jamii bila kujali shule wanakosomea wanafunzi.

“Tuliwaongoza na kufuatilia kuhakikisha hawapotoki, kuozwa mapema na tabia nyingine zizofaa.Ushindi huu unaonyesha walimu barani Afrika wanaweza kufanya makubwa kupitia ushirikiano,” asema Bi Kimiti aliyetangazwa mshindi Disemba 21.

Stephen Wamukota, 9, alivumbua mashini ya kuosha mikono.

Mnamo Juni, Stephen Wamukota, mvulana mwenye umri wa miaka 9, kutoka kijiji cha Mukwe, kaunti ya Bungoma alivumbua mashini ya kuosha mikono kuepusha watu wengi katika maeneo ya umma kushika sabuni na mifereji.

Uvumbuzi wake ambao imetumiwa na mafundi kuunda mashini sawa, ulisaidia kupunguza hatari ya kusambaa kwa virusi vya corona. Habari zake ziliangaziwa na vyombo vya habari kote ulimwenguni.

“Ilikuwa furaha sana kuona mwanangu akifanya jambo la kusaidia umma. Uvumbuzi wake ulifanya mashini sawa kuundwa kote nchini. Wanahabari wa kimataifa walifika na kuangazia habari zake hadi akapata tuzo la Uzalendo,” asema babake James Wamukota.

Amina Ramadhan, polisi mwenye utu

Ingawa maafisa wa polisi walilaumiwa kwa kutumia nguvu kupita kiasi wakitekeleza amri ya kutotoka nje usiku ilipotangzwa Machi mwaka huu kuzuia msambao wa virusi vya corona, mmoja wao aligusa wengi kwa kuwasaidia akina mama waliochelewa kufika nyumbani.

Amina Mutio Ramadhan, aliyehudumu katika kituo cha polisi cha Embakasi, Nairobi aliwasaidia akina mama na watoto wao wakati wenzake walikuwa wakiwadhulumu raia.

“Kama mama na afisa wa polisi, niko na jukumu la kuhakikisha usalama wa kila mmoja. Polisi hutumia nguvu panapohitajika na sio kila wakati. Kuwa na utu ni muhimu,” asema Amina.

Wahudumu wa afya

Katika mwaka ambao corona ilitishia kuangamiza binadamu wote Kenya na ulimwenguni, watu wakiwa nyumbani kwa hofu, wahudumu wa afya walikuwa msitari wa mbele kukagua, kupima, kutibu na kuhamasisha watu jinsi ya kujikinga na virusi vya corona.

Baadhi yao waliambukizwa virusi hivi wakihudumia wagonjwa ambao walinusurika.

Priscilla Kioko, Rebecca Mutua, Faith Mailu

Japo maafisa wengi wa polisi walilaumiwa kwa kutendea raia ukatili wakitekeleza kanuni za kuzuia msambao wa corona, wanawake hawa watatu walijitolea kuwapikia chakula maafisa waliokuwa kwenye kizuizi eneo la Komarock kwenye barabara ya Nairobi,Kangundo.

Maafisa hao waliokuwa wakizuia wakazi kuingia jiji la Nairobi lilipofungwa baada ya maambukizi kuongezeka hawakuwa na mbinu ya kupata chakula baada ya hoteli kufungwa.

Juhudi zao za kuonyesha utu ziliwafanya kukabidhiwa tuzo za Uzalendo mwaka huu. Bi Mailu anasema hawakutarajia kutambuliwa kwa kuwa lengo lao lilikuwa kuwaepusha maafisa hao kuumia kwa njaa wakiwa kazini wakati biashara nyingi zilikuwa zimefungwa.

“Tulitumia mapato yetu kwa shughuli hiyo hadi kizuizi hicho kilipoondolewa,” asema Bi Mailu.

Akothee alilipia kodi wasanii

Msanii Esther Akoth maarufu Akothee alijitolea kuwasaidia wasanii wenzake walioshindwa kulipa kodi ya nyumba na kupata chakula wakati shughuli za burudani zilipigwa marafuku kufuatia janga la corona.

Aliguswa na hali ngumu ambayo wasanii hao walikuwa wakipitia. Aidha alitoa misaada ya chakula kwa wakazi wa maeneo tofauti nchini kupitia wakfu wake wa Akothee Foundation.

“Niliguswa moyo kuona wasanii wenzangu wakiathirika kiasi cha kulala njaa na nikajitolea kuwafaa kwa kidogo nilichopata waweze kulipa kodi na kupata riziki hata kwa siku moja. Siku yangu ya kuzaliwa ilikuwa Aprili na niliamuautu kusaidia wakazi wa baadhi ya maeneo kama Kilifi ambao walikuwa wakiteseka,” asama Akothee ambaye ni mwanachama wa kamati ya kukabiliana na corona ya kaunti za Ziwa Victoria.

Brigid Kosgei, aliwika London Marathon

Alishinda mbio za London Marathon mwaka huu mnamo Oktoba 4 ingawa ulikuwa mwaka mgumu kwa wanamichezo baada ya shughuli za spoti kusimamishwa.

Benard Sang, Diana Chemtai, walishinda Istanbul Marathon

Wanariadha wengine wa Kenya waliowika ziliporejelewa ni Benard Cheruiyot Sang na Diana Chemtai Kipyogei ambao walishinda makala ya 42 ya mbio ndefu za Istanbul nchini Uturuki mnamo Novemba 4.Felix Kimutai, alikuwa wa pili nyuma ya Sang kwenye mbio hizo.

You can share this post!

Serikali yaonywa dhidi ya kuhujumu mahakama

Ruto kuhudhuria sherehe za ushindi Msambweni leo