Na SIMON CIURI
WATOTO watano wamefariki eneo la Mwihoko katika eneobunge la Ruiru, Kaunti ya Kiambu baada ya kutumbukia katika shimo la majitaka la kimo cha futi 20 walipokuwa wanacheza.
OCPD wa Ruiru OCPD, Bw Phineas Lingera amethibitisha na kuambia Taifa Leo kwamba watoto hao waliokuwa wa umri wa kati ya miaka mitatu na saba walitumbukia katika shimo hilo lililokuwa limefunikwa na majani lakini likabomoka.
Shimo hilo lilikuwa limejaa maji kufuatia mvua inayoendelea kunyesha na hivyo afisa huyo anashuku huenda watoto hao walipata matatizo ya kupumua.
“Watoto walikuwa wakicheza karibu na eneo la mradi wa ujenzi na walipokanyaga hapo palipo na shimo la choo, walitumbukia ndani na kufariki kwa kushindwa kupumua,” amesema Bw Lingera.
Maiti za watoto hao kutoka familia tofauti zimepelekwa katika mochwari ya Hospitali ya Chuo Kikuu cha Kenyatta.
Mkasa wa Mwihoko umetokea miezi michache tu baada ya watu watano kufariki eneo la uchimbaji mawe Juja, Kaunti ya Kiambu.