• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 8:27 PM
CHOCHEO: Kupata mchumba si muujiza, lazima utoke ukutane na watu

CHOCHEO: Kupata mchumba si muujiza, lazima utoke ukutane na watu

Na BENSON MATHEKA

NICK anakumbuka Januari 4 mwaka uliopita kama jana.

Ni tarehe ambayo pasta wa kanisa lake alimtabiria kuwa kabla ya mwaka kuisha, angepata muujiza kwa kujaliwa mke anayetamani.

“Aliniambia kwamba ningepata muujiza kwa kujaliwa mke ninayetamani. Nimekuwa nikisubiri muujiza huo na sijapata,” asema Nick akizama kwenye mawazo.

Mwaka umeisha na ni bayana kuwa barobaro huyu mwenye umri wa miaka 27 hatapata muujiza ambao amekuwa akisubiri. Faith Karimi, naye amekuwa akisubiri muujiza ajaliwe mume jamali, mwenye nidhamu na uwezo wa kifedha.

“Ninajua muujiza utatokea na nitajaliwa mume wa ndoto yangu,” asema mwanadada huyu mwenye umri wa miaka 30.

Wanasaikolojia wanasema kwamba japo ni vizuri mtu kuwa na imani kwa Mungu, kutafuta mume au mke hakuwezi kuwa muujiza.

“Ikiwa kuna mhuburi aliyekutabiria uketi kitako ukisubiri upate mume au mke kimiujiza, utasubiri milele. Hauwezi ukapata mchumba kwa kuketi tu. Ni lazima utoke, ukutane na watu, urushe na kurushiwa misitari, uchunguze tabia za watu nao wachunguze zako. Hakuna muujiza katika kutafuta mchumba wa maisha,” asema Daisy Simon wa shirika la Big Hearts jijini Nairobi. Mtaalamu huyu anasema baadhi ya wahubiri na hata waganga wamekuwa wakipotosha watu kwa kuwapa matumaini hewa ya kupata wachumba.

“Badala ya kuambia mtu asubiri muujiza wa kujaliwa mchumba, mshauri anavyoweza kupata mchumba mzuri. Mpe ushauri wa kiroho ajue jinsi ya kuchagua na kujua mtu anayeweza kuwa mume au mke mwema,” asema Daisy.

Kulingana na Steve Keli, mshauri wa wanandoa katika kituo cha Life Center, baadhi ya watu huwaelewa vibaya wahubiri wanapofunza kuhusu miujiza ya kupata wachumba.

“Huwa wanawapa matumaini wale ambao huenda wanakaribia kuvunjika moyo kwa kukosa wachumba lakini baadhi ya watu huchukulia ujumbe huo kuwa utabiri wa moja kwa moja kwamba Mungu atawateremshia wachumba kutoka mbinguni,” asema Keli.

Hata hivyo anakiri kwamba baadhi ya wahubiri huwa wanatoa mafunzo ya kupotosha kwa wanaosaka wachumba. Daisy anasema kanisa ni miongoni mwa maeneo salama ya watu kutafuta wachumba.

“Asilimia kubwa ya watu wanaooana hupatana kanisani au katika shughuli za kanisa. Wengine huwa wanapatana katika shughuli za kikazi au maeneo ya kazi. Kuna wanaokutana katika shughuli za kijamii na burudani. Bidii huwa inahitajika kwa kurusha misitari na kujukumika ili kuinasa roho ya mtu,” aeleza Daisy.

Wataalamu wanasema kuwa ni lazima mtu amshawishi mwingine kwamba atakuwa mke au mume mwema jambo ambalo haliwezi kutendeka kimiujiza. “Kuna kutoka na kukutana na mtu akuvutie, uanze kumvuta karibu nawe na hii inahitaji maombi, bidii, wakati na pesa. Inahitaji kujitoa mhanga sana. Kutafuta mke au mume hakuwezi kuwa muujiza baadhi ya watu wanavyodhani,” asema Keli.

Doreen Kuria, aliyefunga ndoa juzi anasema ilimchukua miaka mitatu kukubali kwamba alikuwa amepata mchumba aliyetamani.

“Mtu akikwambia utapata mchumba kimiujiza anakupotosha. Ni kazi inayohitaji bidii na kujitolea kwingi. Kwanza, ni kibarua kumfahamu vyema mchumba wako hadi uridhike ana sifa unazotaka. Wengine huwa wanajifanya,” asema.

Mwanadada huyu anawashauri watu kutokimbilia miujiza inayonadiwa na wahubiri au waganga wanapotafua wachumba.

“Watu wamepotoshwa na waganga eti watawafanyia vimbwanga wapate wachumba wenye sifa wanazotaka, wengine wamepotoshwa na mafunzo ya kidini hadi wakatulia kusubiri wachumba wawajie. Hizi ni porojo. Omba, amini, chukua hatua kwa hiyo imani. Jipambe na uwe tayari kwa gharama ya kutafuta mchumba kwa sababu ipo na anayekueleza vingine anakundanganya,” asema

You can share this post!

Ratiba ngumu kwa Juventus mnamo Januari 2021. Je,...

Real Madrid watandika Celta Vigo ugani Bernabeu na kurejea...