• Nairobi
  • Last Updated March 19th, 2024 2:13 PM
Shirika lataka IEBC izuiwe kukagua saini

Shirika lataka IEBC izuiwe kukagua saini

Na BRIAN OCHARO

SHUGHULI za uthibitishaji saini za wapigakura kuhusu mchakato wa Mpango wa Maridhiano wa BBI, huenda ikakumbwa na changamoto baada ya shirika moja la kutetea haki za binadamu kuishtaki Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC).

Katika kesi iliyowasilishwa katika mahakama ya Mombasa, shirika la Muslims for Human Rights (Muhuri), linasema kuwa tume hiyo haijaweka wazi mambo maalum ya kisheria na kikatiba yanayoiwezesha kuendesha zoezi la uthibitishaji wa saini.

“IEBC haina hifadhi ya data inayofaa ya wapiga kura kwa ajili ya kutekeleza shughuli hiyo kama inavyotakiwa na katiba,” Muhuri inasema.

Ombi hilo linatokana na mawasiliano kati ya shirika hilo na tume hiyo, ambapo IEBC imeshindwa kutoa majibu ya kuridhisha kwa maswali yake.

Shirika hilo mnamo Desemba 15 liliwasilisha ombi kwa tume hiyo likitafuta maelezo kuhusiana na utaratibu huo wa uthibitishaji saini.

Shirika hilo lilitaka kujua kiwango cha pesa zilizotengwa kuendesha shughuli hiyo.

Katika barua hiyo, shirika hilo lilitaka kujua ikiwa kulikuwa na kanuni au miongozo ya kuendesha mchakato wa uthibitishaji wa saini na pia ikiwa IEBC ina nakala za saini wapiga kura wote waliosajiliwa.

Lakini katika majibu yake, tume hiyo ilisema haina hifadhi ya data ya saini za wapigakura waliosajiliwa, na kuongeza kuwa inahifadhi tu taarifa kuhusu wapigakura waliojiandikisha.

Shirika hilo linasema kuwa katika majibu ambayo IEBC iliipatia, ilizungumza tu juu ya taratibu ambazo imeweka katika shughuli hiyo bila ya kutoa maelezo zaidi jinsi taratibu hizo zitatumika katika uthibitishaji wa saini.

Hazina ya Kitaifa imeidhinisha IEBC kutumia Sh93.7 milioni kwa zoezi hilo. IEBC ilianza mchakato huo mnamo Desemba 30, mwaka jana.

Shirika hilo linashangaa jinsi IEBC itakavyothibitisha saini milioni 4.4 bila hifadhi ya data ya saini za wapigakura wote waliosajiliwa, ambayo imekiri kwamba haina.

“Kwa hivyo mwenendo wa IEBC kuendelea kutekeleza zoezi la uthibitishaji bila hifadhi ya data ya kuaminika ya saini za wapigakura na mfumo wa kuridhisha wa udhibiti wa viwango vya uhakiki ni ukiukaji wa mamlaka yake ya kikatiba.”

Pamoja na mapungufu haya, shirika hilo linasema kuwa kesi yake inastahili kupewa kipaumbele na kusikizwa.

Shirika hilo sasa linataka IEBC izuiliwe kuthibitisha Mswada wa Sheria ya Katiba ya Kenya (Marekebisho) ya 2020 uliowasilishwa kwake na jopo la BBI mnamo Desemba 10.

Pia, Shirika hilo linataka IEBC na Mwenyekiti wake Wafula Chebukati au maafisa wake wazuiliwe kuthibitisha au kuthibitisha kuwa hati hiyo inakifikia matakwa ya Kifungu cha 257 (4) na (5) hadi mfumo kamili wa kisheria, pamoja na kanuni zinazoongoza shughuli hiyo kubuniwa.

Kesi hiyo imeratibiwa kusikizwa Januari 14.

You can share this post!

Biden ampa Trump kichapo cha mwisho kura za useneta

AKILIMALI: Ni mashine ya kisasa ya kuchuma chai, lakini...