Na CHRIS ADUNGO
MECHI za robo-fainali za kuwania taji la Koth Biro mwaka huu zimepangiwa kuanza Jumamosi ya Januari 9 hadi Jumatatu ya Januari 11, 2021.
Kubanduliwa kwa mabingwa watetezi Kingstone FC kutoka Shauri Moyo na vigogo Umeme Bees kunamaanisha kwamba mshindi wa muhula huu atakuwa limbukeni kabisa.
Kingstone FC na Umeme Bees waliagana mashindano hayo mwaka huu kwenye hatua ya 16-bora mnamo Januari 5, 2021 ugani Ziwani, Nairobi.
Kingstone walibandulia na Leeds United ya Kawangware kwa kichapo cha 2-1 huku Umeme wakipokezwa kichapo cha 5-3 kutoka kwa limbukeni Ruaraka All Stars kupitia penalti baada ya pande hizo mbili kuambulia sare ya 2-2 mwishoni mwa muda wa kawaida.
Bingwa mwingine wa zamani aliyedenguliwa kwenye hatua ya 16-bora ni Kaloleni Black Mamba waliopokezwa kichapo cha 2-0 kutoka kwa Terror FC ya Mwiki.
Ijumaa itakuwa siku ya mapumziko kwa washiriki wote kabla ya kushuka dimbani kunogesha mechi za hatua ya nane-bora kuanzia Jumamosi hadi Jumatatu.
DROO YA ROBO-FAINALI:
Kajiado All Stars na Dallas All Stars
Ruaraka All Stars na Leeds United
Githurai United na Terror Squad
Asec Huruma na Biafra FC