Na MARY WANGARI
TUMEKUWA tukiangazia aina mbalimbali ya malipo yanayotumika katika shughuli mbalimbali za kijamii.
Hii leo tutaendeleza mada hiyo kwa kuangazia na kuchambua kwa kina ada hizo mbalimbali jinsi ifuatavyo:
Mahari – Ni malipo yanayotolewa ili kuoa mwanamke au kuolewa na mwanamme kuambatana na jamii husika.
Mwago – Ni malipo kwa mke wa kwanza yanayotolewa na mume anapomletea mke mwenza au ukipenda anapooa mke wa pili.
Tapisho – Haya ni malipo yanayotolewa kwa ngariba kwa ajili ya utahirishaji.
Fichuo – Haya ni malipo au zawadi anayopatiwa mvulana anapotoka jandoni.
Kudu – Haya ni malipo yanayolipwa na mwari kwa nyakanga wake kama adhabu kwa kukosa adabu akiwa unyagoni.
Ridhaa – Haya ni malipo anayopatiwa mtu aliyevunjiwa heshima au hadhi yake.
Hongo, rushwa, chirimiri,mvugulio, kadhongo, chauchau, kilemba – Haya ni malipo au zawadi anayotoa mtu ili kupata kwa njia haramu kitu au huduma asiyostahili.
Arshi au Dia – Haya ni malipo anayopatiwa mtu anayejitolea kutolewa damu.
Kilemba – Hii ni ada, malipo au zawadi za harusi wanazopatiwa wajomba wake bibiharusi. Pia ni malipo yanayotolewa na mwanafunzi kwa mhunzi wake baada kuhitimu mafunzo yake.
Bakora – Ni zawadi anayotoa mzazi kwa fundi akitaka mtoto wake afundishwe ufundi.
Mrabaha – Haya ni malipo anayopatiwa mwandishi na kampuni iliyochapisha kazi yake kila baada ya muda fulani wa mauzo. Pia ni pato au faida inayotokana na biashara.
Mchango – Ni malipo anayotoa mtu kwa hiari kwa mtu anayehitaji au kwa kufanya shughuli fulani kama vile kugharamia bili ya hospitali, ujenzi wa shule na kadhalika.
Fungule – haya ni malipo yanayotolewa kwa daktari.
Bahashishi – Hii ni zawadi anayopatiwa mtu kwa huduma bora, utumishi au kazi aliyofanya.
Kombozi au kiokozi – Haya ni malipo yanayotolewa kukombolewa kitu au mtu aliyetekwa nyara.
Urithi au urathi – Hii ni mali inayoachwa na marehemu na kupatiwa mtu fulani kama vile mtoto au mke wa marehemu.
Rehani – Haya ni malipo ya kitu kilichowekwa dhamana ili kikombolewe baadaye.
Kodi au pango – Hii ni ada au malipo ya nyumba au chumba kilichokodishwa yanayolipwa kila mwezi au baada ya kila muda na mpangaji kwa mpangishaji.
Honoraria – Haya ni malipo au kiasi fulani cha pesa anazolipwa mtu kama bakshishi kwa kazi maalum aliyofanya.
Bakshishi – malipo ya kuonyesha shukrani.
Thawabu – Haya ni malipo anayopata mtu kutoka Maulana kwa sababu ya kutii amri zake na kwa mema aliyofanya.
Rada – haya ni malipo kutoka kwa Maulani kama adhabu kwa mtu kw maovu aliyofanya.
Mapoza – Ni malipo anayopatiwa mtu aliyekwazwa ili kuondoa hasira yake.
Haka – Ni malipo yanayotolewa na jamaa kwa familia yake ili kufidia kosa alilotenda.
Natija, tija au faida – Hizi ni pesa za ziada anazopata mfanyabiashara.
Posho, marupurupu – haya ni malipo ya ziada anayopata mfanyakazi zaidi ya mshahara au ujira wke wa kawaida.
Karisaji – Ni malipo au ada ya muda uliopita.
Kiangazamacho, kiokozi, chorombozi, machorombozi, utotole – Ni zawadi au malipo anayopatiwa mtu kwa kugundua kitu au kushuhudia jambo fulani likitendwa wakati fulani.
Fola – Haya ni malipo au zawadi inayotolewa ili kumshika mtoto mchanga kwa mara ya kwanza.
Ukonavi, kipamkono, kipakasa au jazua – Haya ni malipo au zawadi anayopatiwa biharusi anapoonwa kwa mara ya kwanza.
Kikunjajamvi – Hii ni ada inayoweza kuwa pesa taslimu au mifugo wanayotozwa wafanyabiashara au wakazi wa mabaraza ya kizamani na ya kiasili.
Mukafaa – Ni malipo ya mshahara kwa mfanyakazi kutokana na faida iliyopatikana.
Mbiru – Haya ni malipo yanayotolewa kwa serikali kutokana na mishahara ya wafanyakazi wake.
Zaka au fungu la kumi – Hii ni asilimia kumi inayotolewa na waumini kutoka kwa mapato yao kama ishara ya shukrani kwa Mola.
Fungule – Haya ni malipo ya kwanza yanayotolewa kwa mganga au mpiga ramli.