• Nairobi
  • Last Updated April 18th, 2024 9:15 PM
Njama ya Joho, Kingi ‘kupiga chobo’ vinara wa Tangatanga

Njama ya Joho, Kingi ‘kupiga chobo’ vinara wa Tangatanga

Na CHARLES LWANGA

MIBABE wa chama cha ODM eneo la Pwani sasa wamepanga njama kuwapiku wafuasi wa Naibu Rais William Ruto eneo hilo, wanaotaka kubuni chama kipya cha Wapwani.

Gavana wa Mombasa, Bw Hassan Joho, na mwenzake wa Kilifi, Bw Amason Kingi, wametangaza mipango ya kuzindua chama ambacho Wapwani watajitambulisha nacho kuanzia uchaguzi wa 2022.

Tangazo lao kwamba watazindua chama hicho mwezi Juni, lilikujia saa kadha baada ya wafuasi wa Dkt Ruto katika ukanda huo wametia moto wito wa kubuni chama cha Wapwani.

Mwishoni mwa wiki, Mbunge wa Malindi, Bi Aisha Jumwa, alifichua kuwa chama cha Kadu Asili ndicho wamepiga msasa ili wakitumie katika chaguzi zijazo, bila kutegemea vyama ambavyo vigogo wake si Wapwani.

Lakini Bw Joho alipinga mpango wa Bi Jumwa na wenzake akidai ni mbinu ya kutia kura za Wapwani katika kapu moja kwa manufaa ya Dkt Ruto.

Mnamo Jumamosi katika mazishi ya aliyekuwa mbunge wa Kaloleni, Gunga Mwinga, Gavana Kingi – ambaye ni mwandani wa Bw Joho – alisema eneo hilo lina kura takribani milioni tatu na wakati umefika kwao kujisimamia kisiasa.

“Nataka kuhakikishia wakazi wa Pwani kuwa ifikapo Juni mwaka huu tutakuwa na chama chetu wenyewe ambacho kitaongoza kampeni za uchaguzi,” akasema.

Wakati huo huo, Bw Kingi alikashifu viongozi wa Pwani kwa kupigana wenyewe kwa wenyewe akisema hicho ndicho kizuizi kikuu cha umoja wa kanda hiyo.

“Changamoto kubwa tuliyonayo ni kwamba hata tukiitisha umoja wa Wapwani tunaendelea kupigana wenyewe kwa wenyewe kisiasa, na hata kupigia debe wagombeaji wa kutoka maeneo mengine ya Kenya,” alieleza.

Wiki mbili zilizopita, wabunge wa Tangatanga walimuidhinisha Gavana wa Kwale, Bw Salim Mvurya, kama kinara na msemaji wao eneo la Pwani.

Lakini Jumatano iliyopita wabunge 25 na waziri msaidizi wa usalama, Bw Hussein Dado, wakiandamana na Bw Joho eneo la Garsen kupigia debe Mpango wa Maridhiano (BBI), walimuidhinisha Bw Joho kama kinara na msemaji wao atakayeunganisha Pwani.

Akizungumza katika hafla hiyo, Bw Joho alisema wakati umefika Wapwani pia wasikizwe na maeneo mengine ya Kenya na kufanya misimamo yao wenyewe ya kisiasa.

“Wakati umefika kufanya uamuzi wetu kisiasa. Tumekuwa tukitumiwa na watu kwa manufaa yao; wakati wa kuwa wafuasi wa watu wengine umepita,” akasisitiza.

Alisema matumaini yake kwamba Kiongozi wa ODM Raila Odinga ataunga mkono mgombeaji urais kutoka Pwanii, kwani eneo hilo limemuunga mkono kwa miaka mingi.

“Kuna wale wanadai ati tunataka kiti cha naibu waziri mkuu, hayo si kweli kwa sababu tunalenga kiti cha urais,” alisema.Bw Joho alisema watajaribu mahojiano na wapinzani wao Pwani ili wawarudishe upande wao na wasonge pamoja nao kwa madhumuni ya kuunganisha eneo zima.

You can share this post!

Matiang’i kupewa fimbo ya kuongoza jamii ya Gusii kisiasa

LEONARD ONYANGO: Serikali ina mengi ya kujifunza kuhusu...