• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 12:48 PM
WANTO WARUI: Kuzuia wanahabari shuleni kunaficha maovu

WANTO WARUI: Kuzuia wanahabari shuleni kunaficha maovu

NA WANTO WARUI

Hatua ya hivi juzi ya Wizara ya Elimu kupiga marufuku vyombo vya habari shuleni huenda ikasababisha hasara zaidi kuliko faida.

Ingawaje kwa upande mmoja vyombo vya habari vinaweza kuzusha hali ya taharuki shuleni hasa wakati huu tunapokumbwa na janga la maradhi ya Covid-19, lakini pia kuna maovu mengine sugu ambayo huenda yakafanyika shuleni na yakakosa kumulikwa.

Kuporomoka kwa madarasa ya shule ya Talent Academy ambapo wanafunzi kadhaa walipoteza maisha yao, kwa mfano, ni tukio ambalo lilifungua serikali macho.

Aidha wawekezaji wengine katika sekta hii ya elimu walichukua tahadhari kutokana na kisa hicho. Kama si vyombo vya habari kuangazia suala hilo, huenda kufikia leo wanafunzi wengine wengi wangekuwa wamepoteza uhai wao kutoka na ulegevu kama huo wa wamiliki wa shule.

Mfano mwingine wa maovu yanayoendeshwa shuleni ni kuadhibu wanafunzi kwa kuwatandika kinyume cha sheria. Aidha wanafunzi wengi hasa wale wa kike hupitia dhuluma za kimapenzi ambazo zahitaji kuwekwa wazi ili jamii iweze kukosoa matendo kama hayo. Kumekuwa na kesi nyingi shuleni za mioto na hata matumizi ya dawa za kulevya.

Hofu kubwa ya Wizara ya Elimu katika suala hili ni taharuki inayoweza kuzushwa na vyombo vya habari endapo kutatokea mkurupuko wa maradhi ya Covid-19 shuleni.

Bila shaka ni kweli kuwa jambo kama hilo linaweza kuzua wasiwasi mwingi sana kwa walimu, wanafunzi na zaidi kwa wazazi. Hata hivyo, mtu akificha mwiba na kutoung’oa hatimaye mwiba huo hutunga usaha na maumivu zaidi.Je, serikali imebuni mikakati bora ya kukabiliana na hali ya Covid-19 endapo ugonjwa utakurupuka shuleni?

Ni vipi wengine watajua na kuweza kuchukua tahadhari hasa jamii ambayo inaweza kuwa imezingira shule iliyoathirika?Ni kweli kama alivyosema Waziri wa Elimu kuwa wanafunzi ni wengi zaidi na hawawezi kutoshea madarasa yaliyoko katika shule zetu. Ikiwa kabla maradhi ya Covid-19 hayajaingia madarasa yalikuwa hayatoshi, sembuse sasa?

Ni wazi kuwa sheria ya kujikinga na maradhi haya ambayo ni kutokaribiana ndiyo ngumu zaidi kutekelezwa kwa wanafunzi. Sidhani kuna shule hata moja nchini ambayo itaweza kuhakikisha wanafuzi hawagusani hasa uwanjani wanapocheza.

Jambo la muhimu zaidi ambalo Wizara ya Elimu ingefanya ni kuwaita waandishi wa habari na kufikia muafaka wa mazungumzo nao ili kuwaelekeza yale ambayo wasingependa yawasilishwe hewani huku wakipatia vyombo hivyo fursa ya kukagua maendeleo ya masomo au upungufu wa kimaadili katika shule.Kwa kufanya hivyo, maovu mengi ambayo yanaweza kutokea shuleni yatapunguzwa.

Hali ilivyo sasa, huenda kuna mambo mengi sana mabaya ambao hayatajulikana au kuweza kurekebishwa.

You can share this post!

LEONARD ONYANGO: Serikali ina mengi ya kujifunza kuhusu...

TAHARIRI: Viongozi wetu wachunge ndimi zao