• Nairobi
  • Last Updated March 29th, 2024 9:50 AM
Tangatanga wamzomea Uhuru kwa matamshi

Tangatanga wamzomea Uhuru kwa matamshi

Na WANDERI KAMAU

WANASIASA wa mrengo wa ‘Tangatanga’ wanaomuunga mkono Naibu Rais William Ruto, wamkashifu vikali Rais Uhuru Kenyatta wakidai matamshi yake Jumamosi, kwamba wakati umewadia kwa jamii zingine kuongoza nchi, ni kuchochea ukabila.

Rais Kenyatta alitoa matamshi hayo kwenye mazishi ya mamake kiongozi wa chama cha Amani National Congress (ANC), Bw Musalia Mudavadi, Kaunti ya Vihiga.

Ni kauli ambayo ilionekana kumlenga Naibu Rais William Ruto, ambaye amekuwa akiendesha kampeni kuwa sasa ni wakati wa watu wa tabaka la chini maarufu kama “Hustler Nation” kuchukua uongozi wa nchi.Lakini jana, wabunge zaidi ya 20 wa mrengo huo walikosoa matamshi ya Rais Kenyatta, wakisema yeye binafsi hakuchaguliwa kama rais kwa msingi wa kabila lake.

“Rais Kenyatta lazima afahamu alichaguliwa na Wakenya 2013 na mara mbili mnamo 2017 kutokana na sera alizokuwa nazo kuiendesha nchi wala si kutokana na kabila lake,” akasema Seneta Kipchumba Murkomen wa Kaunti ya Elgeyo Marakwet.

Viongozi hao walikuwa wamehudhuria ibada ya Jumapili katika kanisa la House of Hope, eneo la Kayole, eneo bunge la Embakasi ya Kati, Nairobi, wakiandamana na Dkt Ruto.

Mbunge Rigathi Gachagua (Mathira) alisema ni makosa kwa Rais Kenyatta kuirejesha nchi kwenye mwelekeo huo, ikizingatiwa kesi zilizowakabili pamoja na Dkt Ruto katika Mahakama ya Kitaifa ya Uhalifu (ICC) nchini Uholanzi zilitokana na mapigano ya kikabila mnamo 2007.

Kwa upande wake, Dkt Ruto alisisitiza kuwa Wakenya hawatakubali kurejeshwa katika mijadala ya kikabila, kwani wameona athari zake kwenye chaguzi za awali.

You can share this post!

TAHARIRI: Viongozi wetu wachunge ndimi zao

Sonko agundua kumbe Nairobi ina wajanja kumliko