• Nairobi
  • Last Updated April 16th, 2024 7:55 AM
Walinzi na wafuasi wa Bobi Wine wakamatwa, siku mbili kabla ya uchaguzi

Walinzi na wafuasi wa Bobi Wine wakamatwa, siku mbili kabla ya uchaguzi

Na CHARLES WASONGA

MGOMBEAJI wa upinzani nchini Uganda Bobi Wine Jumanne alifichua kuwa wanajeshi wa serikali walivamia nyumbani kwake na kuwatia mbaroni walinzi na wasaidizi wake siku mbili kabla ya wapiga kura kuelekea debeni kushiriki uchaguzi mkuu.

“Leo asubuhi wanajeshi walivamia nyumbani kwangu na kuwakamata walinzi na mtu yeyote waliyempata karibu,”  Wine, ambaye ndiye mpinzani mkuu Rais wa sasa Yoweri Museveni katika uchaguzi huo wa Januari 14, 2021, alisema kupitia akaunti yake ya twitter.

Mgombeaji huyo ambaye jina lake halisi ni Robert Kyagulanyi alisema hakuna maelezo yaliyotolewa kuhusu sababu ya kukamatwa kwa wasaidizi wake.

Wandani hao wa Wine, 38, ambaye pia ni mwanamuziki mtajika, walikamatwa wakati ambapo mwanasiasa huyo alikuwa akihojiwa na mwanahabari wa Kenya Jeff Koinange katika kituo cha redio cha Hot 96 FM.

Makoa makuu ya polisi na jeshi nchini Uganda hayajatoa kauli zozote kuhusu kisa hicho

Jumla ya wapiga kura 18 milioni nchini Uganda ambao wamesajiliwa wanatarajiwa kushiriki uchaguzi huo wa urais na ubunge mnamo Alhamisi.

Wine ndiye anapigiwa upatu zaidi miongoni mwa wagombeaji urais 10 wanaompinga Rais Museveni ambaye amekuwa mamlakani tangu 1986.

Museveni mwenye umri wa mika 76 amelaumiwa kwa kutumia wadhifa wake kuwadhulumu wapinzani wake na vyombo vya habari.

Kiongozi huyo mkongwe amekuwa wakitumia vikosi vya usalama kuendeleza kampeni za kupambani na wapinzani wake tangu kampeni za kisiasa zilipoanza mwaka jana.

Tangu Novemba 2020 zaidi ya watu 60 wameuawa katika makabiliano kati ya wafuasi wa wagombeaji wa upinzani haswa wale wa Bw Wine. Vitendo hivyo vimelaaniwa ndani ya nje ya Uganda wagombeaji wa urais wa upinzani wakitaka serikali ya Museveni ichunguzwe kwa makosa ya uhalifu dhidi ya binadamu.

Wiki jana, Wine aliitaka Mahakama ya Kimataifa ya Uhalifu (ICC) kumchukulia hatua Rais Museveni kuhusiana na vitendo hivyo vya ukiukaji wa haki za kibinadamu.

Lakini Rais huyo ametetea maafisa wa usalama akisema wamekuwa wakikabiliana na wafuasi wa upinzani wanaokiuka masharti ya kuzuia msambao wa Covid-19 kwa kuandaa mikutano mikubwa ya kisiasa.

Bobi Wine mwenyewe amewahi kukamatwa mara kadhaa wakati wa kampeni na kufikishwa kortini kwa kile maafisa wanasema ni makosa ya kuvunja masharti ya janga la corona.

Mara si moja Museveni amekuwa akishutumu Wine kwa kumtaja kama “mtu anayetumiwa kuendeleza masilahi ya wageni.” Hata hivyo, hajawaji kutoa ushahidi wa kuthibitisha madai hayo.

You can share this post!

Jinsi ya kujitengenezea chokoleti nyumbani

Afueni kwa shule 6 kufunguliwa baada ya miaka saba