• Nairobi
  • Last Updated March 29th, 2024 11:38 AM
Jeshi lamwagwa miji mikuu uchaguzi mkuu ukinukia

Jeshi lamwagwa miji mikuu uchaguzi mkuu ukinukia

NA MASHIRIKA

JESHI la Uganda limeimarisha usalama jijini na nje ya Kampala kabla ya uchaguzi wa urais na bunge uliopangiwa kufanyika kesho. Wanajeshi wanashika doria barabarani huku wengine wakidhibiti hali katika mitaa inayofahamika kama maeneo hatari ya vurugu.

“Muda wa kampeni unaelekea kufika kikomo na sasa tunasonga katika hatua nyingine ya kupiga kura. Sasa tumeimarisha usalama wetu na kuwatuma maafisa wa polisi ambao wanasaidiwa na jeshi. Usalama ni muhumi kuhakikisha haki ya kila mtu kupiga kura na kudumisha imani katika uchaguzi salama na wazi,” Msemaji wa Polisi Jijini Kampala Patrick Onyango, alieleza vyombo vya habari nchini humo.

Aidha, kuna idadi kubwa ya polisi na jeshi wanaotumia magari kushinda ilivyowahi kushuhudiwa katika msimu wa uchaguzi katika taifa hilo la Afrika Mashariki.’

“Kuna makundi ya maafisa wa usalama wanaopiga doria kwa miguu, pikipiki na magari. Tumefanya mazoezi kuhusu matukio kadhaa ikiwemo ghasia za kikatili, makundi ya vijana wenye itikadi kali, dhuluma za kimtandao, mapigano kati ya makundi hasimu na kadhalika. Timu hizo zitakabiliana na aina yoyote ya dharura,” alisema.

Wakuu wa mashirika ya kulinda usalama mnamo Ijumaa yalitoa onyo kwa wote wanaopanga kusababisha vurugu wakati na baada ya uchaguzi kwamba wataadhibiwa ipasavayo.

Adolf Mwesige, waziri wa ulinzi na masuala ya wanajeshi waliostaafu alisema, wagombeaji wa kisiasa ni sharti wakubali uamuzi wa watu utakaotangazwa na Tume ya Uchaguzi.

“Mchakato wa pekee tu unaoweza kutumia kupinga matokeo ni mahakama wala si vurugu. Hii si mara ya kwanza kwetu kushiriki uchaguzi,” alisema Mwesige.

Mashirika ya kigeni nchini humo tayari yametahadharisha raia wake kuwa waangalifu zaidi wakati na baada ya uchaguzi, yakionya dhidi ya uwezekano wa kuzuka kwa ghasia za uchaguzi.

“Polisi kwa kawaida huwa wanatumia nguvu kupita kiasi, ikiwemo vitoa machozi, risasi za mipira na risasi halisi kutawanya maandamano. Maandamano Uganda huenda yakasalia jambo la kawaida na kuna uwezekano wa michafuko kuzidi,” Ubalozi wa Amerika uliwatahadharisha Waamerika ukiwahimiza kuepuka maandamano na mikusanyiko ya watu.

Kipindi cha kampeni za urais kilichoanza mwanzoni mwa Novemba na kukamilika jana Januari 12, kimeandamwa na ghasia mbaya za kikatili ambazo baadhi zimesababisha vifo.

Kukamatwa kwa mgombea urais wa chama cha upinzani, Robert Kyagulanyi mnamo Novemba 18 kulizua maandamano katika baadhi ya sehemu za nchi hiyo na kusababisha vifo vya watu 54 waliouawa na maafisa wa usalama.

Rais aliye mamlakani kwa sasa, Yoweri Museveni alipokuwa akizungumza kuhusu maandamano hayo alijutia vifo hivyo akiahidi kuanzisha uchunguzi.

You can share this post!

Amerika mbioni kumtimua Trump

Mbunge amtaka Joho ajiuzulu ODM