• Nairobi
  • Last Updated March 18th, 2024 8:55 PM
CHARLES WASONGA: Ni aibu sana Rais na Naibu wake wake kupakana tope hadharani

CHARLES WASONGA: Ni aibu sana Rais na Naibu wake wake kupakana tope hadharani

Na CHARLES WASONGA

ILIKUWA makosa makubwa kwa Naibu Rais William Ruto kumjibu hadharani bosi wake, Rais Uhuru Kenyatta, kufuatia kauli ya kiongozi huyo wa taifa kwamba watu kutoka jamii zingine wanapasa kupewa nafasi ya kuliongoza taifa hili 2022.

Rais Kenyatta ambaye alikuwa akihutubu Jumamosi katika kaunti ya Vihiga alipohudhuria mazishi ya mamake kiongozi wa ANC, Musalia Mudavadi, Mama Hanna Atsianzale Mudavadi, aliripotiwa kudai, kimzaha, kuwa jamii mbili za Kikuyu na Kalenjin ambazo zimewahi kutoa marais wa taifa sasa zinapasa “kutoa nafasi kwa watu kutoka jamii zingine kuongoza.”

Lakini Jumapili akihutubu katika kanisa moja mtaani Kayole Nairobi, Dkt Ruto (anayetoka jamiii ya Kalenjin) alilaani tamko hilo akisema linachochea ukabila na migawanyiko nchini, kwa imani kuwa kauli ya Rais ililenga kuvuruga ndoto yake ya kuingia Ikulu 2022.

Kimsingi, ikiwa ni kweli kwamba Rais Kenyatta alitoa kauli kama hiyo, basi alipotoka kwa sababu Katiba haina kipengele kinachosema kiti cha urais kinapasa kushikiliwa kwa mzunguko miongoni mwa makabila ya Kenya.

Isitoshe, Katiba ya sasa (katika kipengele cha 38) inalinda haki ya Wakenya kufanya maamuzi ya kuchagua viongozi wanaowataka bila kushurutishwa kwa misingi yoyote ile.

Hata hivyo, endapo Dkt Ruto alihisi kukerwa na kauli ya bosi wake kile angefanya ni kumfikia kwa njia ya simu na kuwasilisha lalama zake.

Aidha, anaweka kukutana naye katika Ikulu na kuwasilisha hisia zake kwa faraghani. Hakupasa kumjibu hadharani alivyofanya kanisani.Vilevile, hakufaa kuwaachilia wabunge na maseneta 20 walioandamana naye kumkaripia kiongozi wa taifa hadharani walivyofanya ndani ya kanisa hilo la House of Hope.

Ingawa Rais Kenyatta, kama mwanadamu, anaweza kukosea kimatamshi au kwa vitendo, Dkt Ruto kama naibu wake hafai kumkosoa hadharani. Hii ni kwa sababu afisi ya urais ni yenye heshima na taadhima kando na kwamba ni nembo na ishara ya umoja wa kitaifa.

Ni wazi kwamba Rais Kenyatta alitoa kauli hiyo kujibu propaganda ambazo zimekuwa zikienezwa na Dkt Ruto pamoja na wandani wake kwamba wakati umewadia kwa watu wa tabaka la chini, almaarufu, mahasla, kupewa nafasi ya kuliongoza taifa hili na wala sio viongozi ambao wazazi wao waliwahi kuongoza Kenya.

Tasnifu yangu ni kwamba Rais Kenyatta na Dkt Ruto wanapasa kukoma kulumbana hadharani kwani wanajiaibisha machoni pa Wakenya waliowatwika jukumu la kuwaongoza kwa kuwapa kura zao miaka ya 2013 na 2017.

You can share this post!

Mbunge amtaka Joho ajiuzulu ODM

KING’ORI: Shule za mashinani pia zilindwe dhidi ya...