• Nairobi
  • Last Updated April 24th, 2024 10:08 PM
WALLAH BIN WALLAH: Usitumie nguvu za kifua unapofanya kazi, ni akili tu!

WALLAH BIN WALLAH: Usitumie nguvu za kifua unapofanya kazi, ni akili tu!

NA WALLAH BIN WALLAH

KATIKA maisha ukitumia akili kidogo tu vizuri utafanya kazi kubwa vizuri bila kuchoka wala kuumia. Lakini ukitumia nguvu nyingi za kifua bila kutumia akili wakati unapofanya kazi, utachoka, utaumia na kutokwa jasho chapachapa bila kufanikiwa!

Nguvu pekee za kifua hazitoshi kuleta mafanikio katika kila kazi! Kufanya kazi si vita! Lakini hata vita huhitaji akili za kukabiliana na adui! Mafanikio katika utendakazi huhitaji akili na umakinifu zaidi kuliko nguvu nyingi zinazotokana na ugali!

Kila mtu anamjua ndama mtoto wa ng’ombe. Ana ujeuri na kiburi si haba! Akiamua kusumbua wakati akishalala juani, humwamshi, humbebi wala humtikisi atikisike!

Huyo ndiye ndama kwa wanaomjua ndama kuandamana na tabia za ndama!Bwana Tutufe alimtuma mwanawe mvulana aitwaye Tuletule aende akamlete ndama wao aliyelala njiani kwenye jua umbali wa mita mia tatu kutoka nyumbani.

Tuletule kijana wa kidato cha tatu alienda kifua mbele mpaka alikolala ndama! Akajaribu kwa uwezo wake wote kumwamsha ndama lakini ndama hakunyanyuka!

Alijitahidi kwa nguvu zake zote lakini ndama alijipweteka pwetepwete bila kunyanyuka angalau sentimita moja! Alijaribu kumbeba lakini ndama hakubebeka kutokana na uzito wake! Tuletule alitokwa jasho na kuishiwa nguvu!

Alirudi nyumbani akamwambia baba yake, ‘Nimeshindwa kumleta ndama nyumbani!’Bwana Tutufe alimwambia Tuletule, ‘Unakula kama ndovu lakini huna nguvu za kumleta ndama tu nyumbani kutoka juani!!? Twende tukamlete!’ Walipofika mahali alipolala ndama, walijitahidi kumnyanyua lakini ndama alikatalia chini!

Wakaamua kutumia nguvu nyingi zaidi! Baba akamkamata ndama kwa masikio yake amvute. Naye mwana Tuletule amsukume ndama nyuma kwa nguvu zake zote! Walipojaribu hivyo ikawa kazi ngumu zaidi! Waligundua kwamba ndama alikuwa akiumia sana! Alianza kutoa sauti ya kutisha na kukoroma kana kwamba alikaribia kufa!

Walimwachilia alale chini! Wakasimama kumtazama tu huku jasho likiwatiririka baba na mwana!!Mara alifika msichana mdogo aliyetoka sokoni na kikapu chake mgongoni, jina lake Esha!

Baada ya salamu, Esha aliwauliza Baba na Mwana, ‘Ndama ana shida gani?’ Walimjibu juu juu, ‘Amekataa kuenda nyumbani!’ Esha akaomba, ‘Niwasaidie?’ Hawakumjibu, lakini Esha alimkaribia ndama akaweka kidole chake kwenye mdomo wa ndama yule!

Ndama alitoa ulimi akaramba kidole cha Esha! Akanyanyuka na kuanza safari akimfuata Esha unyounyo huku akimramba kidole mpaka nyumbani!!Ndugu wapenzi, tusidhani kazi zote lazima zifanywe kwa kutumia nguvu za kifua tu!

Ukitumia nguvu nyingi bila akili utaumia lakini kazi haitafanyika! Lakini ukitumia akili kidogo tu utafanya kazi kubwa kuliko kutumia nguvu nyingi uchoke bure!!!!

You can share this post!

KING’ORI: Shule za mashinani pia zilindwe dhidi ya...

Olunga ayoyomea Qatar ‘kumumunya mamilioni’