• Nairobi
  • Last Updated March 29th, 2024 8:50 AM
CHOCHEO: Mume si suti, ni ujasiri!

CHOCHEO: Mume si suti, ni ujasiri!

NA BENSON MATHEKA

Faiza alishangaza marafiki wake kwa kumuacha Ali na kumchumbia Abdul ingawa mwanamume huyo alikuwa akimpenda na kumtunza vyema. Kwa mwanadada huyu, hakupata alichotafuta kwa mume katika Ali.

“Ni kweli ana pesa, ni jamala, nadhifu na ananipenda lakini ni mwoga. Siwezi kuishi na mume mwoga katika maisha yangu. Nani atanilinda nikiwa hatarini?” ahoji Faiza.

Mwanadada huyu anasema ingawa Abdul hana pesa kama Ali, ni jasiri. “Ninataka mume ambaye nitahisi kuwa salama sio mwoga atakayeniuliza atakachofanya kunitoa kwenye hatari,” asema.

Sally, mwanadada mwenye umri wa miaka 32 anasema aliolewa na Mwangi kwa sababu ya ujasiri wake. “Nilimuacha mwanamume aliyekuwa akinipatia chochote kwa sababu niligundua alikuwa mwoga.

Ingawa Mwangi ana pesa nyingi, ninajua kitu kimoja, kwamba hakuna anayeweza kunigusa kwa sababu ataona moto,” asema.Wataalamu wa masuala ya mapenzi wanasema kwamba hakuna mwanamke anayeweza kukubali mwanamume mwoga.

“Wanawake hupenda wanaume wanaoweza kuwahakikishia usalama wao, sio tu kwa kukidhi mahitaji yao, mbali pia kuwalinda dhidi ya hatari inayoweza kuwakabili. Unaweza kumpa mwanamke kila kitu anachohitaji lakini ikiwa hauwezi kumlinda akikumbwa na hatari, atakuacha,” asema Steven Omboki, mwanasaikolojia wa kituo cha Abundant Life mjini Athi River.

“Kigezo muhimu ambacho wanawake wanazingatia wanapotafuta mume ni ujasiri. Mtu jasiri anaweza kufanikiwa katika mambo mengi. Hata akishindwa anaweza kupigana hadi afaulu,” aeleza.Kulingana na Martha Kawira, mshauri mwandamizi wa shirika la Maisha Mema, wanawake wanaamini kwamba mwanamume mwoga hawezi kuwa mume bora.

“Kwa wanawake, mwanamume mwoga hafai kuwa mume wa mtu. Woga unafanya mwanamume kukosa mke kwa sababu wanawake wanapenda mtu atakayewahakikishia usalama wao na watoto wao,” asema Kawira.

Daisy Mukami, mwanadada mwenye umri wa miaka 32 na mama ya watoto wawili, asema alimuacha mumewe alipogundua alikuwa mwoga.

“Hakuweza kuua hata panya katika nyumba yetu. Hakuweza kukabili majirani wakituchokoza. Hakuweza kutetea mali yake ikitumiwa vibaya na watu wengine. Hivyo niliamua kumtema kwa sababu kuwa naye ni sawa na kuishi katika nyumba bila mlango,” asema Mukami. Kawira asema mume anafaa kuwa mlinzi wa mke, watoto na mali.

“Mume sio suti, mume ni zaidi ya kuwa na gari, sura nzuri na kumnunulia mkewe zawadi. Mume ni ngao ya mkewe na familia. Ukipungukiwa na ujasiri, unajiweka katika hatari ya kukosa mke,” asema Kawira.

Watalaamu wanasema wanawake wanaofahamu vigezo halisi vya mume bora huwa wanachunguza iwapo wanaowachumbia ni jasiri.

“Mwanamume jasiri huwa anajiamini na kwa kufanya hivyo, anaweza kufanikiwa. Mwanamume jasiri anaweza kuwa mfano mwema kwa wanawe,” aeleza Omboki.

Lakini Kawira anashauri wanawake kutofautisha aina za ujasiri akisema wanaweza kudhani mwanamume ni jasiri lakini awe katili.

“Hata unapotafuta mwanamume jasiri, chunga usiangukie katili atakayefanya maisha yako kuwa jehanamu. Wanawake wengi huwa wanakosea na hatimaye kujuta,” aeleza Kawira.Omboki anakubaliana na kauli hii akisema baadhi ya wanawake huwa wanajuta kwa kuolewa na wanaume katili wakidhani wamepata walio jasiri.

“Ni muhimu kufahamu chanzo cha ujasiri wa mtu. Kuna ujasiri unaotokana na elimu, mali, imani ya dini na kuna ujasiri wa kipumbavu pia wa kutumia kifua. Kuna watu jasiri lakini hawana hekima. Hao ni hatari,” aeleza.

Kulingana na wataalamu, mume anafaa kulinda mke lakini sio kuwa tishio kwake. Damaris* mwanadada mwenye umri wa miaka 28 anasema alidhani mumewe angekuwa ngao yake lakini akamkosesha amani kwa kumdhulumu kila wakati.

You can share this post!

FATAKI: Nani kasema mwanamke hana haki ya kukata kiu ya...

Polisi akana kumuua mwenzake kituoni