• Nairobi
  • Last Updated April 19th, 2024 1:14 PM
FAUSTINE NGILA: Kukwamilia WhatsApp ni ithibati Afrika haitambui usiri wa data

FAUSTINE NGILA: Kukwamilia WhatsApp ni ithibati Afrika haitambui usiri wa data

Na FAUSTINE NGILA

JE, umehama kutoka mtandao wa kijamii wa WhatsApp? Iwapo ungali kwenye jukwaa hilo linalomilikiwa na Facebook, basi wewe ni mmoja miongoni mwa mamilioni ya Waafrika ambao wanapenda kuanika usiri wao.

Wiki iliyopita, WhatsApp ilitangazia watumizi wake kwamba itakuwa ikitumia data zao za siri kuporomosha matangazo katika mitandao ya Facebook na Instagram.

Ilionya kwamba wale ambao hawatakubali sera hiyo mpya basi hawatapata huduma walizozoea.Waafrika wengi wanaipenda WhatsApp sababu ya urahisi wa matumizi, unaowawezesha kuunda vikundi vya siri vya kupiga soga au hata kufanya mazungumzo ya kikazi.

Hata hivyo, mtandao huo hauwezi kuaminika tena kulinda data ya watumizi wake zaidi ya bilioni mbili. Alipoona kuwa Facebook inawanyanyasa wateja kwa kurina data bila ruhusa yao, na kisha kuitumia kibiashara kuunda matrilioni ya hela kupitia matangazo ya mitandaoni, Afisa Mkuu Mtendaji wa kampuni ya magari ya kielektroniki ya Tesla, Bw Elon Musk, aliwaomba walimwengu kugura WhatsApp mara moja na kujiunga na mtandao wenye huduma sawa wa Signal.

Kufikia leo, mamilioni ya watu bara Amerika, Ulaya, Asia na Australia wamejiondoa kutoka WhatsApp na kujisajili katika Signal – ambayo imeweka sera thabiti za kulinda data ya watumizi dhidi ya wizi au matumizi yasiyoruhusiwa.

Ninapotazama kwenye programu yangu ya Signal, wengi wa watumizi wanatoka mabara hayo, licha ya kuwa na nambari za simu za watu kutoka Afrika zipatazo 3800 huku 400 pekee wakiwa wa ughaibuni. Kwa simu yangu, Waafrika ambao wamechangamkia Signal ni 83 pekee, Wazungu ni 289.

Hii ndiyo taswira kamili ya jinsi Afrika ilivyo. Watu wasiojitambua kama wa maana, watu wasiojali data yao ikitumiwa visivyo, watu wanaotegemea mno uvumbuzi wa ughaibuni, watu wanaopenda kuelekezwa kuhusu wanachopasa kufanya, watu wasiojielewa.

Ni wakati wa kung’amua kuwa masoko ya dijitali katika mataifa yaliyoendelea tayari yamefurika.Hivyo, unapoona Facebook ikishurutisha watumizi kukubali sera hasi za kuwakandamiza, basi inalenga Afrika ambako soko bado li wazi kwa uwekezaji wa mabilioni ya dola.

Afrika bado ndilo bara lililosalia na changamoto nyingi, na kuondoa visiki hivi kunahitaji data na taarifa za mambo wanayofanya wananchi wake kuwekwa siri.

Kupata data hii hakufai kuwa jambo la utani bali ichukuliwe kama bidhaa ya kibiashara, ambapo Facebook lazima iwalipe watumizi wake kwa kuchanganua data kuhusu maisha yao.

Utajihisi vipi ukipata mnaso wa simu (screenshot) wa arafa zote ambazo umetuma na kupokea kwenye WhatsApp, ukisambaa mitandaoni? Wasichojua Waafrika wengi ni kuwa, kando na arafa, programu za Facebook husikiliza maongezi ya simu.

Kumaanisha hata wakati hautumii simu, bado inafuatiliwa kana kwamba wewe ni mhuni uliyefanya makosa ya jinai.

Ni wakati wa kugutuka na kufahamu kwamba kukwamilia katika WhatsApp kunaipa Facebook fursa ya kuendelea kukandamiza haki zetu za kimsingi, ambazo zimelindwa katika Sheria ya Ulinzi wa Data ya 2019.

You can share this post!

Jubilee yaachia NASA chaguzi ndogo

WANDERI KAMAU: Uhuru, Ruto wajue dunia nzima inawatazama