• Nairobi
  • Last Updated April 18th, 2024 6:27 PM
WANDERI KAMAU: Uhuru, Ruto wajue dunia nzima inawatazama

WANDERI KAMAU: Uhuru, Ruto wajue dunia nzima inawatazama

Na WANDERI KAMAU

MOJAWAPO ya matukio ambayo daima yatakumbukwa na vizazi vijavyo nchini, ni ghasia za kikabila zilizotokea baada ya uchaguzi tata wa 2007.

Ni machafuko ambayo yalishangaza dunia nzima kwani Kenya ilikuwa imesifika kwa muda mrefu kama taifa linalozingatia demokrasia.Taifa letu linaheshimika sana kote duniani kutokana na uwezo wetu mkubwa na michango muhimu ambayo tumetoa katika nyanja mbalimbali.

Kwa mfano, ufanisi wetu katika riadha umetutambulisha kipekee tangu miaka ya sitin; enzi ambazo watimkaji wakongwe kama Kipchoge Keino, Moses Tanui, Naftali Temu, Douglas Wakiihuri na wengineo walikuwa waking’aa katika mashindano ya kimataifa.

Hatua hizo ndizo zilibadilisha dhana ya wengi, hasa wakoloni, wakatambua kwamba Waafrika si viumbe duni kama walivyofikiria.Wazungu walikuwa wamewadunisha Waafrika tangu karne ya 18 walipovamia bara hili, wakawateka nyara na kuwauza kama watumwa katika mabara ya Ulaya na Amerika.

Hata hivyo, michango muhimu ya Wakenya na raia kutoka nchi zingine za Afrika imegeuza kabisa fikra za Wazungu, kiasi kwamba baadhi yao walianza kubuni mikataba na nchi hizo katika nyanja mbalimbali za ushirikiano, kama vile utafiti wa masuala ya kisayansi.

Umoja wa Mataifa (UN) nao uliweka makao ya Shirika la Umoja wa Mataifa kuhusu Mazingira (UNEP) kuwa jijini Nairobi, kutokana na imani kubwa iliyo nayo kwa Kenya.

Kwa sasa, Kenya inahudumu kwa mara ya pili kama mwanachama wa muda katika Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa (UNSC). Hili ni baada ya kupata uungwaji mkono kutoka nchi nyingi duniani zinazoamini uwezo wake.

Hatua hizi zote zinaashiria kuwa Kenya si nchi yetu tu; bali ni taifa lililo na wajibu muhimu wa kutimiza katika ulimwengu nzima.Kinaya ni kwamba, inashangaza sisi wenyewe hatutambui hilo.

Moja ya dalili ni cheche ambazo viongozi wa kisiasa wameanza kuelekezeana kuhusiana na Uchaguzi Mkuu wa 2022. Sikitiko kuu ni kwamba miongoni mwa wale ambao wameanzisha mwelekeo huu hatari ni Rais Uhuru Kenyatta, Naibu Rais Wiliam Ruto na Kiongozi wa ODM, Bw Raila Odinga.

Uhalisia mwingine mchungu unaoshangaza ni kwamba Rais Kenyatta na Dkt Ruto walikuwa miongoni mwa Wakenya sita waliofunguliwa mashtaka ya uchochezi katika Mahakama ya Kimataifa ya Uhalifu (ICC), jijini Hague, Uholanzi.

Mashtaka hayo ndiyo yalikuwa msingi mkuu wa Muungano wa Jubilee, waliobuni mnamo 2012 na kuahidi kuanzisha mchakato wa kuunganisha nchi.

Maswali yanaibuka: Wamesahau ahadi walizotoa kwa Wakenya? Wamesahau yaliyowakumba binafsi na familia zao baada ya mashtaka hayo?Sijui ikiwa huo ndio ukweli, lakini itakuwa sikitiko kubwa ikiwa ndivyo.

Ni sikitiko pia ikiwa wamesahau kuhusu Wakenya waliomwaga damu na wengine kuachwa bila makao kutokana na mapigano hayo.Ujumbe mkuu wa Rais Kenyatta na Dkt Ruto ni kukumbuka kuwa Kenya si yao pekee, bali ina maslahi ya watu na nchi zingine duniani. Watahadhari wanakotuelekeza!

[email protected]

You can share this post!

FAUSTINE NGILA: Kukwamilia WhatsApp ni ithibati Afrika...

Tuliteua Bi Kavindu kwa misingi ya sifa za uongozi –...