• Nairobi
  • Last Updated March 19th, 2024 7:55 AM
Joto la siasa lapanda Pwani Ruto na Raila waking’ang’ania kura za wakazi

Joto la siasa lapanda Pwani Ruto na Raila waking’ang’ania kura za wakazi

NA MOHAMED AHMED

JOTO la siasa limepanda Pwani huku migawanyiko ikizuka katika kambi za kiongozi wa ODM Raila Odinga na Naibu Rais William Ruto.

Kambi ya Bw Odinga imeingiwa na kiwewe kufuatia tangazo la Gavana Amason Kingi kuwa atazindua chama cha Wapwani kufikia Juni mwaka huu huku mwenzake wa Mombasa Hassan Joho akihimiza umoja wa wakazi.

Mianya pia imeibuka katika kambi ya Dkt Ruto baada ya Mbunge wa Malindi Aisha Jumwa na Owen Baya wa Kilifi Kaskazini kuanza kuvutana kutokana na azma zao za kuwania kuwania ugavana 2022.

Hii ni baada ya Bi Jumwa kutangaza KADU Asili kuwa chama cha Wapwani, naye Bw Baya akitangaza kuwa chama cha wakazi wa mwambao kitazinduliwa mwezi Machi.

Mvutano katika kambi ya Dkt Ruto pia unashuhudiwa Taita Taveta kati ya wabunge Naomi Shaban (Taveta), Jones Mlolwa (Voi) na Lydia Haika (Mwakilishi wa Wanawake).

Joto hilo la siasa kati ya Bw Odinga na Dkt Ruto linasukumwa na ushindani wa kuzoa jumla ya kula milioni 1.7 za eneo hilo, ambapo Tangatanga wamepata matumaini kufuatia ushindi wa mgombeaji wao katika uchaguzi mdogo wa Msambweni, Feisal Bader mwezi uliopita.

Hii imechochea magavana Kingi na Joho kuanza mikakati ya kuzima mawimbi ya Tangatanga eneo la Pwani.

Wachanganuzi wanasema kuwa msukumo wa kubuni chama cha Wapwani ni mbinu ya ODM kukabili upepo wa Dkt Ruto kwa kushawishi wakazi kuunga mkono chama kinachohusishwa nao, kisha baadaye waingie katika muungano na ODM.

Bw Joho anaungwa mkono na maseneta Mohammed Faki (Mombasa) na Stewart Madzayo (Kilifi), pamoja na wabunge Ali Wario (Garsen), Abdulswamad Nassir (Mvita), Mishi Mboko (Likoni), William Kamoti (Rabai), Said Hiribae (Galole), Andrew Mwadime (Mwatate), Omar Mwinyi (Changamwe), Badi Twalib (Jomvu), Ken Chonga (Kilifi South) na Teddy Mwambire (Ganze).

Wengine ni wabunge waakilishi wa wanawake, Gertrude Mbeyu (Kilifi), Aisha Mohammed (Mombasa) na Ruweida Obbo (Lamu).Mrengo wa Tangatanga nao una aliyekuwa seneta wa Mombasa Hassan Omar na wabunge Mohamed Ali (Nyali), Jumwa (Malindi), Khatib Mwashetani (Lunga Lunga), Benjamin Tayari (Kinango), Baya (Kilifi North), Paul Katana (Kaloleni), Ali Wario (Bura), Shariff Athman ( Lamu Mashariki), Feisal Bader (Msambweni) na wabunge waakilishi, Bi Haika (Taita Taveta) na Rehema Hassan (Tana River).

Mchanganuzi wa siasa za Pwani, Profesa Hassan Mwakimako anapuzilia mbali juhudi za viongozi wa mirengo hiyo miwili akisema wote wanasukumwa na maslahi yao ya kibinafsi wala sio kwa ajili ya wakazi.

You can share this post!

Nitapinga matokeo uchaguzi ukikosa uwazi – Bobi Wine

Wakenya kuumia zaidi bei ya mafuta kipanda tena