• Nairobi
  • Last Updated March 29th, 2024 11:38 AM
Mshindi wa urais Uganda kujulikana kesho

Mshindi wa urais Uganda kujulikana kesho

NA DAILY MONITOR

TUME Huru ya Uchaguzi nchini Uganda inatarajiwa kumtangaza mshindi wa kiti cha Urais hapo Jumamosi baada ya kuandaa uchaguzi wake mkuu Alhamisi.

Sheria ya tume hiyo inasisitiza kuwa matokeo ya uchaguzi lazima yatangazwe saa 28 baada ya upigaji kura kumalizika. Shughuli za uhesabu wa kura bado zinaendelea kote nchini na matokeo ya awali yanaanza kupokelewa leo kutoka vituo mbalimbali vya kupiga kura.

Zaidi ya wapigakura milioni 18 walimiminika katika vituo mbalimbali kumchagua Rais mpya huku ushindani mkali ukitarajiwa kuwa kati ya Rais Yoweri Museveni na Mwanasiasa mwanamuziki Robert Kyagulanyi maarufu kama Bobi Wine.

Huduma za mitandao nazo zilisalia kuzimwa kwa siku ya pili mfululizo hatua iliyochukuliwa na serikali ili kuzuia raia kueneza habari ambazo zingezua taharuki na ghasia.

Pia kulikuwa na visa vya mashine za kielektroniki za kuwatambua wapigakura kufeli kufanya kazi katika Wilaya ya Wakiso na pia masanduku ya kupiga kura yalichelewa kufika katika baadhi ya maeneo ya mashinani na hata kwenye baadhi ya vituo jijini Kampala.

Katika kituo cha polisi Gayaza, shughuli za upigaji kura hazikuwa zimeanza kufikia saa tatu asubuhi baada ya mashine za kielektroniki za kuwatambua wapiga kura kukosa kufanya kazi.

“Nimetembelea vituo vingi vya kupiga kura na hakuna chochote kinachoendelea. Baadhi wameondoka kwa hasira huku wengine nao wakiwazomea maafisa wa uchaguzi,” akasema mmoja wa waangalizi Lydia Ainomugisha.

Katika Manispaa ya Kira, watu walisusia kupiga kura baada ya kugundua masunduku yaliyokuwa na karatasi za kupiga kura yalikuwa yamefunguliwa.

Vijana katika kituo cha Wandegeya, nao walikataa kuwapisha wazee na akina mama wajawazito kutangulia kupiga kura wakisema kuwa hata wao walikuwa na haraka ya kutekeleza majukumu yao ya kikatiba.

“Tumekuwa tukiwaruhusu wazee hawa na akina mama kutangulia kila mwaka wa uchaguzi kisha wanawapigia kura viongozi wakongwe wasiotusaidia kitu. Leo hatutawahurumia wazee hao kwa sababu watakufa hivi karibuni na kutuacha hapa tukiteswa na viongozi hao ilhali wao ndio waliwachagua. Tumekuwa tukiwaheshimu lakini leo wapange laini au warejee nyumbani,” akasema kijana mmoja.

Hapo Alhamisi, usalama uliimarishwa katika vituo mbalimbali vya kupiga kura hasa jiji la Kampala ambalo kwa miaka mingi imekuwa ngome ya upinzani.

Baadhi ya maafisa wa polisi walionekana wakipanda kwenye paa ya majumba marefu wakiwa wamejihami vikali kupambana na utovu wowote wa usalama.

Katika mtaa wa mabanda wa Kamwokya ambako Bobi Wine alilelewa, foleni ndefu zilishuhudiwa huku nao polisi wakiwa ange kuhakikisha kuwa raia wanasimama umbali wa mita moja unusu kuzuia maambukizi ya corona.

“Niko hapa kupiga kura ili kubadilisha uongozi wa nchi. Mara nyingi utawala wa sasa umekuwa ukidai utabadilisha maisha yangu lakini hali bado ni ile ile,” akasema dereva Joseph Ndung’u aliyekuwa kati ya watu wa kwanza kupiga kura.

Mwaniaji huru Henry Tumukunde ambaye alipiga kura yake katika kituo cha Kisementi, jijini Kampala naye alisema hatukubali matokeo hata kabla ya kura kuhesabiwa akisema uchaguzi huo ulijaa udanganyifu.

“Angalia nimepiga kura lakini baada ya kutumia sanitaiza, mkono umekuwa safi na wino umefutika. Watu wanaweza kupiga kura hata zaidi ya mara moja hasa ikizingatiwa mashine nazo zinafeli. Sitakubali matokeo hayo,” akasema.Rais Yoweri Museveni, Wine na wawaniaji wote walipiga kura kwenye uchaguzi huo ambao ulishirikisha nyadhifa za ubunge na udiwani.

TAFSIRI NA CECIL ODONGO

You can share this post!

Wakenya kuumia zaidi bei ya mafuta kipanda tena

Pasta kusubiri Yesu korokoroni