• Nairobi
  • Last Updated April 19th, 2024 10:55 AM
Uhuru hawezi kunisaliti – Raila

Uhuru hawezi kunisaliti – Raila

Na BENSON MATHEKA

KIONGOZI wa chama cha ODM Raila Odinga  amepuuza wanaodai kwamba Rais Uhuru Kenyatta hayuko makini kwa handisheki akisema ana hakika kiongozi wa nchi hawezi kumcheza shere.

Alisema kwamba handisheki yake na Rais Kenyatta ilitokana na mazungumzo ya dhati kati yao na wanaosema kwamba atasalitiwa wanadaganya.

“Tuliketi, tukazungumza kwa muda mrefu kabla ya kusalimiana na Uhuru na hawezi kumsaliti Raila. Tulikuwa wawili, wale ambao walikula kiapa cha urais. Wanaotoa kauli kama hizo ni takataka,” alisema Bw Odinga.

Mnamo Jumamosi, seneta wa Siaya James Orengo alinukuliwa akisema iwapo Jubilee haiko tayari kuadhibu wanaopinga BBI, ODM kiko tayari kuchukua nafasi yake ya upinzani.

Alimlaumu Naibu Rais William Ruto ambaye amekuwa akipinga BBI akisema Rais Kenyatta anafaa kumchukulia hatua kuthibitisha amejitolea kufanikisha BBI.

Akihutubia katika kanisa katoliki la Soweto, mtaani Kayole Nairobi jana, Bw Odinga aliwataka Wakenya wasipotoshwe na Dkt Ruto na washirika wake wa kisiasa wapinge marekebisho ya katiba akisema amezoea kueneza uongo kutimiza maslahi yake ya kisiasa.

Bw Odinga alimtaka Dkt Ruto kutimizia Wakenya ahadi alizowapa wakati wa kampeni za uchaguzi mkuu wa 2017 kabla ya kupinga BBI.

“Kuna watu wanaoeneza porojo na propaganda kuhusu BBI ili wawapotoshwe, msikubali uongo wao kwa sababu amezoea kudanganya,” Bw Odinga alisema.

Aliwakumbusha Wakenya kwamba Dkt Ruto aliahidi Wakenya kwamba serikali ya Jubilee ingetoa vipatakalishi kwa wanafunzi miezi sita baada ya kuingia mamlakani, kujenga viwanja 47 kote nchini ma kubuni nafasi 1 milioni za kazi kwa vijana ambazo kufikia sasa hajatimiza.

“Wakenya hawajasahau ahadi hizo na kwa hivyo haufai kuwaletea ahadi mpya za wilibaro,” alisema.

Bw Odinga aliwaambia vijana kwamba BBI ina mengi ya kuwafaidi na anachofanya Dkt Ruto ni kuwapotosha ili waikatae wasinufaike.

Alisema uongo wa Dkt Ruto umefika ukingoni. “Vijana hawawezi kunufaika kwa kuendesha wilibaro, tunataka kuona Wakenya wanapata ujuzi mpana waweze kujikimu kimaisha,” alisema.

Waziri Mkuu wa zamani alisema BBI itabadilisha uchumi wa nchi kwa sababu itazima ufisadi ambazo viongozi wamekuwa wakipora na kutangatanga nchini wakichanga pesa za wizi.

You can share this post!

Facebook yazima ujumbe wa Uhuru kwa Museveni

Messi apewa kadi nyekundu ya kwanza akichezea Barca